Wednesday, March 16, 2011

MASHUHUDA JITOKEZENI JAMANI MAANA NAJIULIZA HII MIUJIZA YA 'BABU' NI YA KWELI KABSAA AU...

Mchungaji Ambilikile Mwasapile

KAMA kuna tukio ambalo liliwahi kugusa hisia na maisha ya wananchi wengi katika historia ya nchi yetu, basi tukio hilo ni kupatikana kwa dawa inayosemekana inatibu magonjwa sugu na yaliyoshindikana, yakiwamo Kisukari, Kansa na Ukimwi. Hakika, tunashindwa kupata maneno stahiki ya kuelezea jinsi Watanzania walivyopokea habari za kupatikana kwa tiba hiyo iliyoelezwa kupatikana katika Kijiji cha Samunge, wilayani Loliondo, mkoani Arusha.

Ni tukio lililoitikisa na linaloendelea kuitikisa nchi yetu wakati maelfu kwa maelfu ya wananchi, wazee kwa vijana, wanaume kwa wanawake wa itikadi na imani zote wakielekea kijijini Samunge kumuona Mchungaji Ambilikile Mwasapile ili awapatie tiba ya magonjwa hayo sugu. Ndio maana tunasema kuwa hilo ni tukio kubwa na la kihistoria, na ukubwa wa tukio hilo hasa unatokana na ukweli kwamba ni tukio la kiimani.

Kwamba Mchungaji huyo alioteshwa katika ndoto mwaka 1991 kuwa kuna dawa itakayoshushwa kwake ili aitumie kutibu magonjwa ambayo yameshindikana kutibiwa na binadamu. Mashuhuda wengi wanasema walitibiwa na dawa ya mchungaji huyo tangu alipoanza kutoa huduma hiyo mwaka 2009. Baadhi wamejitokeza hivi karibuni na kusema kuwa wamepona maradhi hayo sugu.

Na kama hiyo haitoshi, watu waliopata dawa ya Mchungaji Mwasapile tangu habari za tiba yake zilipochapishwa na gazeti hili kwa mara ya kwanza wiki iliyopita, wamesema dawa hiyo imewatibu na sasa wanaona wako fiti. Baadhi ya madaktari wamethibitisha kuwa wateja wao ambao awali walikuwa wanasumbuliwa na magonjwa hayo wamethibitika kupona baada ya kutumia dawa hiyo inayojulikana kwa jina la Mugariga.

Hicho hasa ndicho kielelezo cha sababu ya maelfu kwa maelfu ya wananchi kumiminika Loliondo wakitokea kila pembe ya nchi yetu wakifuata dawa hiyo inayosemekana ni ya ajabu. Pia hicho ndicho kielelezo cha akili, mawazo, macho na masikio ya Watanzania wote kuelekezwa katika Kijiji cha Samunge na kutekwa na nguvu anayosemekana kuwa nayo Mchungaji Mwasapile.

Na hasa hiyo ndio sababu ya Serikali kujikuta njia panda pasipo kujua la kufanya. Katika kuonyesha hali ya kuchanganyikiwa, Serikali kwanza ilitangaza kupiga marufuku shughuli za Mchungaji Mwasapile na baada ya wananchi kupaza sauti wakitaka huduma hiyo iendelee, Serikali ilisalimu amri mara moja hasa baada ya kutambua kuwa sauti za wananchi zilikuwa za kiimani zaidi.

Ni kwa sababu hiyo tunaipongeza Serikali kwa kutambua kuwa badala ya kuweka vizuizi ili maelfu kwa maelfu ya watu wasifuate tiba hiyo kijijini Samunge, ilikuwa busara kuwawezesha watu wapate tiba hiyo. Serikali ilifanya vyema kugundua kuwa maelfu ya watu waliokuwa wanafuata tiba hiyo wasingeogopa vizuizi au vitisho vyake, kwani baadhi yao walikuwa wamekata tamaa kutokana na maradhi sugu yaliyokuwa yanawasumbua, hivyo walikuwa tayari kwa lolote, hata kufa.

Vilevile, Serikali iligundua kuwa isingekuwa na askari wa kutosha kusimamia amri zake kwa sababu askari wengi walikuwa njiani kuelekea kijijini Samunge na wengine tayari walikuwa wamewasili huko kupata dawa hiyo. Pia, baadhi ya mawaziri, wabunge na watendaji wakuu serikalini walikuwa miongoni mwa wananchi waliokuwa wanafuata dawa hiyo.Ndio sababu tangazo la Serikali kuruhusu shughuli hizo za tiba kuendelea ziliwapa watu wengi faraja na matumaini makubwa.

Sisi tunawahadhalisha wananchi na Serikali kuwa, pamoja na tiba hiyo kuwa suala la kiimani, tusifanye makosa kuanza kufanya sherehe. Tunawashauri wananchi wote kwanza waipe dawa hiyo muda wa kutosha ili itoe matokeo na baadaye wataalamu wa afya wayathibitishe pasipo shaka.

Kwa upande mwingine, tunawashauri wale wanaohisi wameponywa au hawajaponywa na dawa hiyo wajitokeze kutoa ushuhuda ili mamlaka husika ziweze kufanya tathmini na kuwapa wananchi maelekezo stahiki. Ni imani yetu kuwa watakaoponyeshwa na dawa hiyo hawatafanya vitendo hasi, bali watamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwaletea nuru mpya.

No comments:

Website counter