|                            SOKO la Pamoja la Afrika Mashariki limeanza kazi  katika nchi wanachama, changamoto inakuja kwa wajasiriamali ambao hawana  elimu ya kutosha kufanya biashara ndani na nje ya nchi,” anasema  mjasiriamali Peter Mashili.                             |  |                               |                                                                     | Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bariadi, Deogratius Hela akimpongeza Mashili. |  
 |                               |  |                               | 
 |  
 Kauli ya Mashili (45), inatokana na mtazamo wake wa mbele kuhusu  elimu ambapo kwa kutambua umuhinu wake amelazimika kwenda shule licha ya  kuwa na umri mkubwa, ili aweze
 kusimamia vyema biashara zake sambamba na kujiandaa kukabiliana na soko hilo.
 
 Anasema soko hilo linaonekana kuwa tishio kwa wafanyabiashara wa Tanzania ambao wamekuwa wakidai hawajaandaliwa kulipokea.
 
 Anasisitiza kama Serikali haijawaandaa kukabiliana na soko hilo  wafanyabiashara wanatakiwa kuwa na malengo ya muda mrefu pamoja na  kujiandaa na changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wowote.
 
 “Nimeliona hilo na kwa kuwa sikupata nafasi ya kusoma vizuri  nilipokuwa mtoto, niliamua hivyo sasa na nimehitimu kidato cha sita  nitatimiza malengo yangu na familia yangu,”
 anasema Mashili.
 
 Anasema wajasiriamali wasiokwenda shule watapata wakati mgumu katika kulimudu Soko
 la Pamoja la Afrika Mashariki lililoanza hivi karibuni. Mashili amehitimu kidato cha sita katika
 Sekondari ya Hillcrest ya jijini Mwanza, ambapo alikuwa anasoma masomo ya biashara.
 
 Anasema umri sio kigezo cha yeye kutosoma, na kuongeza kwamba  wajasiriamali na Watanzania waoga ambao hawapendi kujiendeleza watapata  wakati mgumu kwenye soko hilo.
 
 “Natoa rai kwa wajasiriamali wenzangu kutoogopa kwenda shule hata kama umri wao ni
 mkubwa, huenda kwa siku za nyuma hawakupata nafasi hiyo kutokana na sababu mbalimbali,
 sasa waamke wasome Elimu haina Mwisho”, ni kauli ya Mashili.
 
 Dunia ya leo ni ya utandawazi, dunia kama kijiji, elimu ya maisha inayopatikana mitaani
 haitoshi ambapo wakati umefika kwa Watanzania kuona kuwa elimu ndiyo msingi wa maisha
 ya kila siku na kulazimika kujiendeleza.
 
 Mjasiriamali asiye na elimu katika Soko la Pamoja atajenga hofu pamoja na kutojiamini,
 hivyo kutoweza kushindana na wajasiriamali wengine, kwa kuwa pamoja na vigezo vya soko
 hilo suala la elimu lina umuhimu wake.
 
 Nchi nyingine zilizoingia kwenye Soko hilo la Pamoja wamepata  maandalizi mapema sambamba na mifumo yao ya elimu lakini hapa kwetu  udhaifu wa lugha ya Kiingereza unatoa
 mwanya kwa wenzetu kupata nafasi zaidi ya kushinda.
 
 Anatoa mfano unapozungumza na raia wa Kenya, mara nyingi hutumia  lugha ya Kiingereza, anapoona unayumba kwenye lugha hiyo, huwa na  wasiwasi ya kutofaa kwenye soko hilo .
 
 Biashara zote hivi sasa zinaendeshwa kwa kusaini mikataba na iwapo  mjasiriamali hana uelewa ni wazi atashindwa kufanya biashara vyema na  kupata hasara kila kukicha ama atalazimika
 kutafuta watu wenye elimu ili waweze kumsaidia.
 
 “Shughuli za kiuchumi ninazofanya zinaambatana na elimu mfano ujenzi, dawa ambapo
 nilibaini kuwepo kwa changamoto hiyo, wakati mwingine ilinilazimu  kusaini mikataba nisiyoielewa mingi imeandaliwa na wenye taaluma au  ufahamu wa lugha,” anasema Mashili.
 
 Huku akionesha furaha yake kwenye mahafali ya kumaliza kidato cha  sita katika shule hiyo, Mashili anasema hivi sasa ana uwezo wa kusoma  nyaraka zote na kuzielewa vizuri kabla ya kuzisaini.
 
 Wakati akisoma shuleni hapo, alimkabidhi mkewe majukumu ya kusimamia shughuli zake
 wakiwamo wataalamu aliowaajiri. Mashili anasema hakubahatika kusoma  elimu ya sekondari akiwa na umri wa kufanya hivyo kama ilivyozoeleka,  kutokana na hali ya uchumi ya wazazi wake.
 
 Hivyo alijikita zaidi kwenye ujasiriamali ambapo alipata fedha ila  kwa kuwa hakuwa na elimu hakuweza kuziendeleza ipasavyo, hadi alipoamua  kurudi darasani. Mwaka 2005 alijiunga na kidato cha kwanza katika  Sekondari ya Bupandagira iliyopo wilayani Bariadi, Mkoa wa Shinyanga  baada ya kupata mafunzo ya Kiingereza.
 
 Mwaka 2008 alihitimu kidato cha nne na kupata daraja la tatu kisha alijunga na Sekondari ya
 Hillcrest kwa masomo ya kidato cha tano na sita kwa mchepuo wa  Biashara. Anasema aliamua kusoma masomo ya biashara ili yamsaidie  kuendesha biashara zake ambapo tayari amezianzisha lakini amelazimika  kuajiri wataalamu wa kumsaidia kutokana na
 kutokuwa na elimu ya kutosha.
 
 Lengo la Mashili ni kufika chuo kikuu na ili aweze kufanya kazi zake kwa ufanisi na uelewa,
 hivyo kutosaini au kudanganywa kwenye nyaraka mbalimbali za  biashara. Anasema akiwa shuleni alipata changamoto mbalimbali kutokana  na umri wake, ambapo wapo baadhi ya wakuu wa shule walimkataa asijiunge  na shule hizo kwa kuwa umri wake ni mkubwa.
 
 Alipopata nafasi kwenye shule hizo,wanafunzi wenzake walimshirikisha kwenye mijadala
 ambayo yeye aliiona kuwa ni ya kitoto na wakati mwingine alikuwa  akipewa chakula kingi ikilinganishwa na wanafunzi wengine kutokana na  umri wake.
 
 Peter Mashili ni mwenyeji wa Wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza na mkazi wa Wilaya ya
 Nzega mkoani Tabora ni mtoto wa saba kati ya watoto 11, wa mzee Andrew Mashili alipata
 elimu ya msingi mwaka 1982 hadi 1988.
 
 
 | 
                   
No comments:
Post a Comment