|  
  Aliyekuwa  ofisa habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Florian Kaijage
 ALIYEKUWA   ofisa habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Florian Kaijage  ametajwa  kuhusika na uzembe uliosababisha fadhaa kwa uongozi wa kitaifa  akiwamo Rais Jakaya Kikwete kwa kutoimbwa nyimbo za mataifa wakati wa  mechi ya kimataifa ya Taifa Stars  na Morocco mwaka jana.
 Akizungumza  na wanahabari jijini Dar es Salaam jana, mwenyekiti wa kamati maalum ya  kuchunguza tukio la kutopigwa nyimbo hizo wakati wa mchezo huo wa  Oktoba 8 mwaka jana, ambaye pia ni Mwanasheria Mkuu wa zamani wa  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), Hamidu Mbwezeleni alisema  wamebaini kuwa  Kaijage alishindwa kutekeleza wajibu wake na hasa baada  ya kupuuza maagizo ya kikao cha maandalizi ya mechi hiyo.
 
 "Kwanza  kabisa tumebaini siku moja kabla ya mechi kulikuwa na kikao cha  maandalizi ya mchezo  kati ya serikali na TFF."Kimsingi,  Rais wa TFF,  Leodegar Tenga alimwagiza Kaijage kuhakikisha CD za nyimbo za taifa  zinaandaliwa mapema na kufanyiwa majaribio ili kama kuna upungufu uweze  kurekebishwa mapema na  ikiwezekana hata bendi ya brass  ya polisi  itumike, lakini hakutekeleza maagizo hayo.
 
 "Pia, mwenyekiti wa  kikao cha matayarisho ya mechi hiyo, Leonard Thadeo (Mkurugenzi wa  Michezo, Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo) aliagiza  uongozi wa Uwanja wa Taifa ufungue mapema milango mapema  kumwezesha  Kaijage na timu yake kufanya majaribio mapema ya vifaa vyote, lakini  Kaijage hakufanya hivyo licha ya milango hiyo kufunguliwa kama  walivyoagizwa," alieleza Mbwezeleni.
 
 Mbwezeleni alilitaja kosa  jingine lililofanywa na Kaijage kuwa ni kumkabidhi mtaalamu wa Kichina  kwenye studio za uwanja huo CD  ya aina ya MP3 ambayo ilikuwa haioani na  mashine zinazotumika kwenye uwanja  huo hali ambayo ilileta mtafaruku  mkubwa.
 
 Mbwezeleni alisema Kaijage baada ya kumpa Mchina CD hizo  aliondoka na kuendelea na shughuli zake nyingine alizokuwa nazo kwenye  Uwanja wa Taifa, lakini Mchina alipojaribu kupiga wimbo huo wa Morocco  CD iligoma kwa sababu ni MP3.
 
 Mtaalamu huyo wa Kichina alipoona  CD aliyopewa haioani na mashine za pale uwanjani aliamua kutoka kwenye  studio na kuanza kumtafuta Kaijage ambaye hakukumwona.
 
 Mbwezeleni  alisema Kaijage alipomaliza shughuli zake alirudi studio ili kuonana na  mtaalamu huyo wa Kichina ili kujua mambo yanakwendaje, lakini Mchina  hakuwepo kwa sababu alikuwa tayari amekutwa na zahama ya CD kukataa  kupiga na alikuwa akimtafuta Kaijage.
 
 " Msimamo wa kamati ni  kwamba Kaijage, ama alikuwa mzembe au hakuwa mwangalifu katika utendaji  wake wa kazi hiyo,"alisema mwenyekiti wa kamati hiyo.
 
 "Tumebaini  kuwa Kaijage hakwenda kufanya majaribio ya CD  kama alivyoelekezwa,  alimkabidhi mtaalamu wa Kichina   CD za MP3 wakati mashine iliyoko  uwakanjani hapo haitumii mfumo huo, hivyo ni dhahiri ulikuwa uzembe kwa  sababu kama angefanya majaribio mapema zipo studio ambazo zimeweza  kutengeneza CD nyingine,"alisema Mbwezeleni.
 
 Aidha, mwenyekiti  huyo alisema kuwa kamati yake imetoa mapendekezo ya kuwepo kwa mtaalamu  wa Kitanzania au Kichina, lakini awepo studio saa moja kabla ya mchezo  kuanza, tena bila kuondoka.
 
 Pia, imependekezwa kuwa watu wa itifaki (protocol) wapatiwe nyimbo za taifa siku moja kabla ya mchezo ili kuzifanyia mazoezi.
 
 Kamati  hiyo, pia imeshauri kwamba suala la mazoezi ya vyombo na mashine za  sauti liwe la lazima na wahusika waandikiwe) na kutaarifiwa kuhusu kazi  hiyo ili kuondoa fadhaa kama ilivyojitokeza.
 
 Katika mchezo huo   wa kufuzu kwa fainali za Afrika mwaka 2012, Stars ilifungwa kwa bao 1-0  huku nyimbo hizo zikilazimika kuimbwa wakati wa mapumziko ya mchezo huo,  jambo ambalo lilisababisha aibu na fadhaa, kiasi cha TFF kuunda kamati  hiyo.
 
 Katika utetezi wake, Kaijage aliiambia kamati hiyo kuwa  alizidiwa na kazi kubwa mbili, zikiwamo za kushughulikia vitambulisho  vya ziada kwa ajili ya waandishi wa habari pamoja na watangazaji wa  kituo cha Supersports cha Afrika Kusini kilichorusha laivu mechi hiyo.
 
 Jukumu  jingine likiwa la kuandaa orodha ya wachezaji wqa timu zote mbili  zilizotakiwa kucheza siku hiyo kwa muda kabla ya kuanza kwa mchezo  huo.Pia, aliieleza kamati kwamba alichelewa kupata CD yenye wimbo wa  taifa wa Morocco hadi Oktoba 8 saa 11.00 jioni.
 
 Kesho yake, yaani  Oktoba 9, Kaijage aliieleza kamati hiyo kuwa alipata CD nyingine ya  wimbo huo kutoka kwa maofisa wa diplomasia wa Morocco waliotokea  Nairobi, Kenya, majira ya saa 4 asubuhi, hivyo kutopata muda wa kutosha  wa kuzifanyia mazoezi ya kutosha.
 
 Kamati hiyo, hata hivyo  haipendekezi hatua zozote za kinidhamu dhidi ya Kaijage, ambaye hata  hivyo ameondoka TFF na nafasi yake  tayari imejazwa na Boniface Wambura.
 
 | 
No comments:
Post a Comment