|  
  Katibu  mkuu wa Chadema Dk Willibroad Slaa akihutubia umati wa watu waliofurika   katika uwanja wa Mkendo mjini msoma jana katika muendelezo wa  maandamano ya chama hicho nchi nzima yalioanzia mkoani Mwanza alhamisi  wiki hii.MAANDAMANO  ya Chadema yameingia mkoani Mara  na kuuteka mji wa Musoma huku Katibu  mkuu wa chama hicho, Dk Wilibroad Slaa, akitoboa siri ya kulipuka kwa  mabomu ya Gongo la Mboto na Mbagala.
 Naye Mwenyekiti Chadema  taifa, Freeman Mbowe aliitahadharisha Serikali kuwa taifa litaingia  kubaya iwapo mchakato wa mabadiliko ya katiba utachakachuliwa kwa maslai  ya mafisadi.
 
 Akizingumza jana katika Uwanjwa wa Mukendo mjini  Musoma baada ya maandamano ya kilomita 15 kutoka Bweri hadi mjini, Dk  Slaa alisema kulipuka kwa mabomu hayo kumetokana na Serikali ya CCM  chini ya Rais Jakaya Kikwete kupuuza ombi la Jeshi la Wananchi wa  Tanzania (JWTZ) kuwapa fedha kwa ajili ya kuteketeza mabomu yaliyokwisha  muda wake.
 
 Alisema kazi ya jeshi ni kulinda uhai wa watu wake  nchini, lakini kupitia jeshi taifa limeweza kupoteza watu zaidi ya 40  kutokana na serikali kugoma kutoa fedha hizo ambazo ziliombwa na JWTZ.
 
 “Tunataka  Kikwete atueleze kwa kina kama ni kweli, maana tunaambiwa kabla ya  mabomu kulipuka mwaka 2009 JWTZ (Mbagala) waliomba fedha kwa ajili ya  kuteketeza mabomu, lakini kutokana na serikali kutothamini maisha ya  watu wake ilikataa kuwa hakuna fedha.
 
 "Tunaambiwa tena kuwa  kabla ya mabomu haya ya mwisho kulipuka wanajeshi waliomba fedha  serikalini kwa ajili ya kuteketeza mabomu hayo, lakini pia serikali  hiyohiyo haikutoa kwa madai kuwa hakuna fedha,” alieleza Dk. Slaa.
 
 Kwa sababu hiyo akamtaka
 Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi alijiuzulu.
 
 Dk  Slaa alisema kuwa Watanzania wanataka Waziri Mwinyi afuate nyayo za  baba yake kama ambavyo alijiuzulu kwa mauaji ya polisi mkoani Shinyanga  na kwamba asipofanya hivyo baada ya siku tisa kuisha Chadema watatangaza  hatua ya pili kwa ajili ya kumshinikiza ajiuzulu.
 
 Onyo kuhusu Katiba
 
 Akizungumza  katika mkutano huo uliokuwa umefurika watu, Mweyekiti wa chama hicho,  Mbowe alitahadharisha kuwa serikali ya CCM itaingilia na kuvuruga  mchakato wa katiba kwa maslai yake binafisi, basi "Tanzania patachimbika  kama Tunisia na Misri."
 
 Hata hivyo, Mbowe alisema kwa muda sasa  amekuwa akishangazwa na kauli za Rais Kikwete ambazo zimekuwa zikidai  kuwa nchini kuna udini akisema hizo ni propaganda zake.
 
 Alisema kama kweli Kikwete anauhakika juu ua jambo hilo basi anapaswa kuwachukulia hatua wahusika.
 
 Kabla  ya mkutano huo viongozi hao waliwaongoza wananchi wa Musoma kuandamana  umbali wa kilomita 15 wakitembea kupinga ugumu wa maisha na kulipwa kwa  Dowans.
 
 
 “Tutaendelea kuandamana mpaka maskini wa Tanzania  asikilizwe. Tutaandamana mpaka vijana wa kitanzania wapate ajira na  hatutalala mpaka kieleweke,” alisema Mbunge wa Ilemela, Highness Kiwia.
 
 Mbunge  wa Nyamagana, Ezekiel Wenje alisema vijana  wengi wanafanya kazi za  umachinga kwa sababu ya mfumo mbovu uliowekwa na serikali unaowafanya  wakose ajira.
 
 “Musoma kulikuwa na kiwanda kizuri sana cha  Mutex kilichokuwa kinatoa ajira kwa vijana, lakini kwa uzembe na ujanja  wakawapa watu kwa madai ya kubinafsisha. Sasa kimefungwa hakuna ajira  kwa vijana na matokeo yake ndiyo wamachinga ambao wanapigwa mabomu kila  wakati,” alisema Wenje na kuongeza.
 
 “Kuna kila sababu ya kutafuta haki kwa njia mbalimbali. Andamaneni mpaka haki yenu ipatikane."
 
 
 Mbunge  wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi alisema Wamarekani wana msemo  kuwa  anayehifadhi magaidi naye ni gaidi, hivyo wasanii wanazunguka na CCM na  kuimba kuwa nchi hii ina amani nao ni wasaliti.
 
 Mbunge wa Kawe,  Halima Mdee alisema pamoja na kuwa jimbo lake linakaliwa na vigogo wote  wa nchi hii, lakini mwaka jana walifikia hatua ya kuikataa CCM.
 
 “Kama  Kawe wamesema CCM baibai inakuwaje ninyi watu wa Mara. Nawaambieni kuwa  mwaka 2015 majimbo yote saba yanatakiwa yachukuliwe na Chadema na  kuingia Ikulu, maana sisi tumewaahidi kupambana na ufisadi mpaka  mwisho," alisema.
 
 Utetezi wa Mbunge Lema
 
 Dk Slaa  alizungumzia pia kitendo cha Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema  kutakiwa kuwasilisha ushahidi kwa madai yakuwa kuwa Waziri Mkuu, Mizengo  Pinda alidanganya bungeni hivi karibuni.
 
 Dk Salaa alisema kuwa  tayari amewasilisha ushahidi na kwamba unaonyesha wazi kuwa Waziri Mkuu,  Mizengo Pinda alidanganya mara 23 bungeni kuhusiana na suala la mauaji  ya Arusha.
 
 “Spika aliomba ushahidi Lema kapeleka, lakini kwa sababu alitaka kumlinda Pinda akasema kuwa ushahidi huo upelekwe kwake.
 
 "Lema  ameitwa muongo hadharani na ushahidi aliowasilisha umebainisha Pinda  ndiye alidanganya mara 23, sasa tunataka apewe nafasi hadharani bungeni  auseme ushahidi wake katika kikao cha bunge lijalo Aprili,” alidai Slaa.
 
 
 | 
No comments:
Post a Comment