Thursday, January 6, 2011

IVI JAMANI TUNAELEKEA WAPI, NA MWISHO WAKE NI NINI HASA...


Viongozi wa Chadema wakiwa katika maandamano jijini Arusha


POLISI mkoani Arusha, jana lilimwaga damu za watu kadhaa, walioshiriki na wasioshiriki maandamano yaliyoandaliwa na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Risasi za moto na mabomu ya machozi vilitumika katika jitihada za polisi kuzima maandamano ya Chadema, wakitekeleza amri ya Mkuu wa Jeshi hilo, Ispekta Jenerali Saidi Mwema.

IGP Mwema alitangaza kuyapiga marufuku maandamano ya Chadema akibainisha kwamba taarifa za kiintelijensia zimebaini kwamba kungekuwa na vurugu wakati wa kufanyika kwake.

"Maandamano hayo ni marufuku, lakini wanaruhusiwa kufanya mkutano wao wa hadhara. Kuna taarifa za kiintelijensia kwamba kunaweza kutokea fujo na uvunjifu wa amani,” alisema IGP Mwema alipozungumza na waandishi wa habari juzi jioni.

Awali Chadema iliruhusiwa kufanya maandamano hayo yaliyoandaliwa kushinikiza taratibu zifuatwe katika uchaguzi wa wenyeviti au mameya wa halmashauri nchini.

Maandamano hayo pia yalilenga kuwahamasisha wananchi wa mkoa wa Arusha na mikoa jirani kushiriki kutoa maoni yao bila woga juu ya kuandikwa upya katiba ya nchi, pindi kamati itakapoanza kazi.

Maandamano hayo yalipangwa kuwashirikisha wabunge wote wa Chadema, na yalipangwa kuanza jana saa 4:00 asubuhi na kuishia kwenye viwanja vya NMB mjini Arusha ambako mkutano wa hadhara ungefanyika.

Kamanda wa polisi mkoa wa Arusha, Thobias Andengeye juzi aliruhusu maandamano hayo lakini akasisitiza kwamba jeshi lake litatoa ulinzi ili kuhakikisha yanakuwa ya amani.

"Tumekubali maandamano na mkutano wa Chadema lakini tunaomba wafuate taratibu na wahakikishe hakuna uvunjifu wa amani ambao unaweza kutokea," alisema Andengenye.

Hata hivyo baadaye juzi jioni IGP Mwema, aliitisha mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam na kutangaza kuyafuta.

IGP Mwema aliwaeleza waandishi wa habari kuwa ameamua kufuta kibali cha maandamano hayo kutoka na kupata taarifa za kiintelijensia kwamba “kungetokea vurugu”.

Mchumba wa Katibu mkuu wa Chadema Dk Willibrod Slaa Josephine Mushumbusi akiwa anavuja damu baada ya kupata kipigo kutoka kwa polisi eneo la tanki la maji jijini Arusha akiwa kweye maandamano jana.

Agizo hilo Jipya la IGP Mwema lilifanya viongozi wa chama hicho kilichojizolea umaarufu, hasa baada ya kuanzisha hoja ya Katiba, kukaidi na kusisitiza kuwa maandamano hayo yangefanya jana kama ilivyopangwa.

Na walipojaribu kufanya maandamano hayo polisi ilianza kutumia risasi za moto na mabomu ya machozi kuwatawanya waandamanaji hao uamuzi ambao ulifanya watu kadhaa wakiwamo wabunge wa Chadema kujeruhiwa vibaya.

Hadi jana jioni zaidi ya watu kumi, akiwepo mke wa Dk Slaa, Josephine Mushumbusi, walijeruhiwa kwa kipigo huku watu wengine watatu, wakiwa wako hoi baada ya kupigwa risasi za moto.

Wakati watu hao wakiumizwa kwa vipigo, mali kadhaa ikiwamo gari la mbunge wa viti maalum mjini moshi, Grace Kiwelu viliharibiwa.

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe pia alikumbwa na dhoruba pale alipojikuta akitumbukia kwenye mtaro wa maji machafu na polisi kumshabulia, wakati alipokuwa akishiriki maandamano pamoja na wabunge kadhaa wa Chadema.

Wakati hayo yakiendelea, shughuli zote katika mji wa Arusha zilisimamia huku barabara kadhaa nazo zikifungwa tangu asubuhi kutokana na vurugu za polisi na kamatakama ya watu iliyokuwa ikiendeshwa na jeshi hilo.

Vurugu za polisi pia zilifika katika makazi ya watu na katika hospitali ya wilaya ya Arusha ya Kaloleni ambako, wagonjwa kadhaa walizimia kutokana na polisi kurusha mabomu ya machozi jirani na hospitali hiyo.

Daktari za zamu wa hospiali hiyo, Anna Kimaro alielezea kushangazwa na hatua ya polisi kurusha ovyo mabomu ya machozi jirani na hospitali.

Baadhi ya wagonjwa, Mwanaidi Mussa na Sabra Khalfani, walisema wamedhurika na hali hiyo kwani walipatwa na mshtuko.

“Mwanangu alipoteza fahamu kabisa hadi sasa hajisikii vizuri,” alisema Sabra alipozungumza na Mwananchi hosipitalini hapo, huku akiwa amebeba mtoto wake Abdul Yusuph, mwenye umri chini ya mwaka mmoja.

Katika vurugu hizo, pia baadhi ya waandishi wahabari walijeruhiwa kwa kupigwa na polisi akiwepo mwandishi wa gazeti hili, Moses Mashala,mpiga picha wa kituo cha televisheni cha Channel ten, Ashraf Bakari, mwandishi wa kujitegemea wa BBC, Moses Kilinga na wengine kadhaa.

Kamanda Andengenye hakupatikana jana kuelezea idadi kamili ya majeruhi kwani polisi, waliwazuia wanahabari kufika kituo kikuu cha polisi huku wakiwataka kuondoka eneo la kituo hicho katika muda dakika tano.

1 comment:

Anonymous said...

Tunaelekea kwenye true FREEDOM na mwisho wake ni kifo kwa mafisadi.

Website counter