Wednesday, December 29, 2010

SIKU CUF WALIPOWAPIGA 'BAO' POLISI...

CUF wawazidi ujanja polisi, waandamana Send to a friend


Wafuasi wa CUFwakiandamana Buguruni jiji la Dar es Salaam jana kuelekea ofisi ya Waziri wa Katiba na Sheria kuwasilisha Rasimu yao ya Katiba mpya. Picha na Michael Jamson


CHAMA Cha Wananchi (CUF) jana kiliwazidi ujanja polisi waliokuwa wakidhibiti maandamano yao baada ya kufanikiwa kuyafanya na kuwasilisha rasimu yao sifuri ya katiba kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria. Polisi hao walikuwa wanazuia maandamano hayo kutekeleza agizo la Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam Suleiman Kova aliyolitoa juzi kuzuia maandamano hayo kwa kile alichoeleza kuwa ni batili.

Katika maandamano hayo yaliyosimamisha kwa muda shughuli za kiuchumi na kijamii, wafuasi na wapenzi wa chama hicho wakiongozwa na Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro, walifanikiwa kuingia barabarani na kuwasilisha rasimu yao ya katiba kama walivyopanga. Hata hivyo maandamano hayo yaliyoanzia Buguruni Sheli hayakuanza saa 2:00 asubuhi kama yalivyopangwa kutokana na mvutano ulioibuka baina ya waandamanaji hao na polisi wenye silaha ambao walifika ofisini hapo kuwadhibiti.

Kabla ya kuanza maandamano hayo, polisi waliwatangazia wananchi hali ya hatari na kuwataka wajifungie majumbani mwao huku wakifyatua risasi za moto na kurusha mabomo kuwatawanya. Gazeti hili lilifika Buguruni Sheli saa 2:00 asubuhi na kukuta eneo hilo limetapakaa askari wa kikosi cha Kuzuia Ghasia (FFU) huku wengi wakiwa wamejipanga katika maeneo mbalimbali ya barabara ya Uhuru kuwazuia waandamanaji.

Ilipofika saa 3:30 asubuhi lilipita gari la matangazo la CUF lenye vipaza sauti na ndani yake kulikuwa na mtu aliyekuwa akitangaza kuwa maandamano yapo palepale na yataanzia Makao Makuu ya Chama, saa 4:30 asubuhi badala ya Buguruni Sheli.

Mara baada ya tangazo hilo, wananchi walianza kukusanyika kwa wingi nje ya makao makuu ya chama hicho wakiwa na mabango mikononi na vitambaa vilivyoandikwa ujumbe mbalimbali wa kudai katiba mpya. Baada ya mabadiliko hayo ya ghafla polisi waliamua kuwafuata kwenye na kuwaonya, “Wanachama wa CUF, maandamano yenu ni batili.

Tafadhali fuateni sheria kuwasilisha madai yenu.” Kauli hiyo ya Dereva wa gari la Polisi aina ya Defenda aliyevalia sare za FFU ilirudiwa mara tatu lakini, wanachama hao hawakusikia badala yake wakaendelea na azma ya kutaka kuandamana huku wakiimba, “Chinja ua, Katiba Lazima.”

Tangazo hilo lilifuatiwa na tangazo la hali ya hatari lililotangazwa na Dereva huyo ambaye alisema “Naomba wenye magari ya kiraia mwende mbele, waandishi wa habari mwende mbele, wananchi ingieni majumbani mwenu na wafanyabiashara fungeni biashara zenu, tunataka kufanya kazi.” Lakini licha ya tangazo hilo la hatari, waandamanaji waliendelea kuimba na kusogelea magari hayo ya FFU zaidi ya matano yaliyokuwa mbele yao.

“Mara ya mwisho, narudia wananchi wa CUF maandamano yenu si halali, fuateni sheria kuwasilisha madai yenu,” alisema dereva huyo ambaye jina wala nambari yake haikujukana huku wanachamahao hao wakimjibu, “Hamtufanyi lolote ninyi.

Kama ni mabomu na maji ya kuwasha tumezoea.” Baada ya hapo magari hayo ya polisi yaliyokuwa yamesheheni askari wenye silaha nzito za moto na mabomu ya kutolea machozi, yaliondoka na kwenda kuegeshwa katika makutano ya barabara ya Uhuru na barabara ndogo inayoingilia Makao Makuu ya CUF eneo la Rozana.

Baadaye waandamanaji walianza maandamano na walipofika Rozana, magari ya polisi yaliondoka na kwenda kuegeshwa katika kituo cha mabasi cha Buguruni Malapa, ambako gari maalumu la kumwaga maji ya kuwasha maarufu kama deraya, lilikuwa limeegeshwa. Baada ya kuona hivyo waandamanaji walijipa moyo na kuona labda polisi wanawaogopa na hivyo kuingia moja kwa moja katika barabara kuu ya Uhuru kuelekea mjini.

Lakini, walipofika Malapa, walikumbana na kizuizi cha magari ya polisi zaidi ya sita ya FFU na deraya nyingine. Hapo ilikuwa kama mchezo wa kuigiza baina ya FFU na waandamanaji, baada ya kila upande kumtunishia msuli mwingine. Wakati polisi wakiwataka wanachama hao wasalimu amri na kusitisha maandamano yao, wanachama hao wanajibu "Kuandamana ni haki yetu kikatiba."

Wakiwa wanatunishiana misuli katika kituo cha mabasi cha Malapa, gari moja la FFU lilikaa katikati ya barabara na dereva wake alitangaza tena “Tafadhali hili gari usilipite, ukilipita hili gari unatafuta shari.” Lakini pamoja na tangazo hilo, wanachama hao waliendelea kulipita gari hilo na mkuu wa operesheni ya polisi hao akaruhusu gari la maji ya kuwasha kuanza kuwarushia maji.

Wakati hayo yakiendelea, daladala na magari yote yanayotoka na kwenda Buguruni yalikuwa yamezuia kupita na kupaki pembeni ama kwa amri au kwa hofu yao wenyewe. Baada ya kuona kizuizi hicho waandamanaji hao waliamua kuingia mitaani na kwenda kuibukia katika mitaa ya Amana na Ilala Boma na kuendelea na safari ya kuelekea Wizarani. Wakati huo polisi walikuwa wameachwa Malapa. Polisi hao walisituka kwamba maandamano yanaendelea wakati waandamanaji hao walipokuwa tayari wamefika eneo la Karume na Mchikichini.

Maandamano yalipofika kati ya mitaa ya Ilala Boma na Karume, polisi hao ambao walikuwa tayari wameshajawa na hasira kwa mchezo wa sinema waliokuwa wakichezewa na waandamanaji, waliamua kufyatua risasi za moto kuwatawanya. Pia mabomu kadhaa ya kutoa machozi yalilipuliwa katika mitaa hiyo jambo ambalo lilisababisha waandamanaji hao kuanza kupoteza mwelekeo huku baadhi ya viongozi wao, wakifanikiwa kupita kwa gari la chama lenye bendera.

Baadaye maandamano hayo yalifanikiwa kufika ofisi za Wizara ya Katiba na Sheria ambako viongozi wa CUF walikabidhi rasimu yao ya katiba. Akizungumza baada ya kukabidhi rasimu hiyo, kiongozi wa maandamano hayo Julius Mtatiro alisema maandamano yalikuwa halali na kwamba licha ya kupigwa mabomu na kutishwa kwa risasi za moto, wamefanmikiwa kufikisha ujumbe kwa serikali na wadau wote wa katiba.

“Tumefanikiwa kufikisha ujumbe wetu ingawa maandamano yetu yalikatiswa na polisi hali ambayo inaonyesha wazi ubakaji wa demokrasia nchini kwani maandamano ni haki ya kikatiba ya kila raia,” alisema Mtatiro. “Tumekabidhi rasimu yetu sifuri ya katiba wizarani, ingawa waziri hatukumkuta lakini tunashukuru imepokewa na katibu mkuu wa wizara hiyo,” aliongeza Mtatiro. Hata hivyo katika makabidhiano ya rasimu hiyo, waandishi wa habari hawakuruhusiwa kuingia ndani ya ofisi na kushuhudia.

Mwisho Juzi Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam Al-hajji Suleiman Kova aliwaeleza wanahabari kuwa maandamano hayo ya Chama Cha Wananchi (CUF), ameyazuia na kwamba ni batili, huku kwa upandeo wao CUF kupitia Mtatiro wakisisitiza kutimiza azma ya kuandamana hadi kwa Waziri Kombani na kumkabidhi rasimu hiyo.


1 comment:

Anonymous said...

Hahaha, wamewaweza kweli, ila siku nyingine msizoee ,mtapigwa mabomu ya moto

Website counter