Thursday, December 30, 2010

JAMANI SASA TUNAZIKWA TUKIWA HAI, MWL NYERERE FUFUKA UONE NCHI YAKO 'INAVYOUZWA' NA WACHACHE DAAH...


AG frederick Werema


MSIMAMO wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema alioutoa juzi kwamba serikali inatakiwa kuilipa kampuni ya kufua umeme ya Dowans Tanzania Ltd fidia ya Sh 185 bilioni umepingwa vikali na baadhi ya wasomi, wanazuoni na wanasaisa nchini.

Kadhalika baadhi ya watu wa makundi hayo tofauti waliozungumza na Mwananchi jana walisema Jaji Werema hana mamlaka ya kutangaza kufungwa kwa mjadala, huku wakihoji ni nani aliyempa mamlaka hayo na kwamba ana maslahi gani katika kampuni ya Dowans.

Ulipaji wa fidia hiyo unafuatia uamuzi uliotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Biashara (ICC Court), Novemba 15, mwaka huu chini ya Mwenyekiti Gerald Aksen na wasuluhishi Swithin Munyantwali, Jonathan Parker ukiamuru Tanesco iilipe Dowans kiasi hicho cha fedha.

Akizungumza juzi katika viwanja vya Ikulu jijini Dar es Salaam mara baada ya kuapishwa kwa Jaji Mkuu mpya, Mohamed Chande Othman, Werema alisema mjadala kuhusu Dowans umefungwa rasmi na kwamba hakuna mpango wa serikali kukata rufaa. Kauli hiyo ya Jaji Werema ni kama imefuta ndoto za Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) ambalo lilionyesha nia kwamba lingechukua hatua za kukata rufaa baada ya uamuzi wa ICC kusajiliwa rasmi katika Mahakama Kuu nchini.

Kadhalika kauli hiyo ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ina uelekeo wa kupinga na na ile iliyotolewa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliyewaambia wahariri wiki moja iliyopita kwamba kulikuwa na mchakato wa kuangalia uwezekano wa serikali kukata rufaa dhidi ya uamuzi huo wa ICC.

Jaji Werema katika maelezo yake alikwenda mbali zaidi akiwabeza wale waliowahi kutoa kauli za kupinga kulipwa kwa Dowans kwa kusema kuwa “Kwa hukumu hii siwezi kusema tutalivalia njuga suala la Dowans maana kwa hukumu hii hata ukiivalia hiyo njuga itafikia mahala njuga hizo zitakatika tu”.

Ni kutokana na kauli hizo tata na nyingine, baadhi ya wananchi wamehoji kile walichokiita utetezi wa Mwanasheria Mkuu kwa kampuni ya Dowans, huku wengine weakidai kwamba huenda ana maslahi katika kampuni hiyo.

Katibu Mkuu Chama cha Chadema, Dr Willbroad Slaa amemtaka Jaji Werema kujiuzulu kutokana na kuweka wazi kwamba serikali itailipa fidia kampuni ya Dowans Tanzania Ltd. Dk Slaa ambaye aliibua mjadala mzito kuhusu kampuni hiyo katika vikao vya bunge mjini Dodoma wakati akiwa mbunge wa Karatu , jana aliliambia gazeti hili kwamba kauli ya Jaji Werema inaonyesha jinsi Tanzania ilivyo kichwa cha mwendawazimu. "Dowans wameingia nchini kwa utaratibu ambao mpaka leo haujajulikana na kurithi mitambo ya Richmond, mitambo ambayo tulizungumza sana kwamba imeingia kwa njia za kifisadi," alisema Dk Slaa, Aliongeza, " Tuhuma za kampuni hii zilikuwa nzito, zimewekwa wazi lakini serikali haijachukua hatua yoyote, kesi hii mpaka imekwenda mahakamani hakuna lolote la kueleweka,".

Alisema kuwa kitendo cha serikali kukubali kuilipa Kampuni ya Dowans kina maana kwamba fedha zitakazolipwa kwa Kampuni hiyo ni za Watanzania na kufafanua kwamba serikali inalipa deni lisilowahusu. "Kauli ya Jaji Werema inaonyesha kwamba yeye na serikali ni wazembe, utatoaje idhini bila kuchunguza jambo husika, kuliko kutoa kauli hii alitakiwa kujiuzulu tu," alisema Dk Slaa. "Nchi hii inaendeshwa vibaya, serikali haiko makini inaipeleka Tanzania sehemu mbaya,". Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Abdallah Safari alisema umefikiwa wakati serikali ikaweka wazi nani ni mmiliki wa Dowans na kuacha kuwaadaa Watanzania.

" Jaji Werema anashindwa nini kuwataja wamiliki wa Dowans, hapa tatizo liko wapi......., mikataba hii iliyojaa rushwa imeibua mijadala mikubwa nchini, sasa ili kuweka mambo sawa watueleze nani mmiliki wa Dowans na serikali inamlipa nani,' alisema Profesa Safari Kwa upande wake Mbunge wa Kigoma Kusini kupitia NCCR Mageuzi, David Kafulila ambaye hivi karibuni alitangaza kusudio lake la kupeleka hoja binafsi katika Mkutano wa Pili wa Bunge, Februari mwakani kutaka serikali iwajibike kwa kuliingiza taifa hasara kwenye sekta ya umeme, kutokana na hukumu ya kesi ya Dowans alisema Jaji Werema “hana ubavu wa kufunga hoja ya Dowans”.

"Hili suala mimi nimeshaliwasilisha bungeni bado kupangiwa siku tu ya mjadala, hapo Werema au serikali haiwezi kuzuia mjadala uliopo bungeni," alifafanua Kafulila. Aliongeza, kuwa Jaji Werema hawezi kufunga mjadala wa hasara ya Sh 185 bilioni na kuongeza kwamba ni lazima aeleze uhalali wa kulipa deni hilo wakati tayari ilishaelezwa mkatabahuo ulikuwa batili. "Serikali imeshindwa kusema hata mmiliki wa Dowans ni nani, sasa inakwenda kumlipa nani, mzimu au, alihoji Kafulila. Alisema ana imani kwamba Spika wa bunge, Anne Makinda atairuhusu hoja yake na kusisitiza kuwa ataweka mambo yote hadharani ili umma wa watanzania ufahamu mbivu na mbichi kwa kuwa hauwezi kuumizwa na madeni kwa mchezo wa serikali dhaifu.

Naye mhadhiri wa chuo hicho katika Shule ya Sayansi ya Siasa na Uongozi wa Umma, Dk Bashiru Ally, alisema inasikitisha kuona mwanasheria mkuu akitoa msimamo kama huo, wakati ofisi yake inahusika na kuisababishia serikali hasara ya bilioni ya fedha kutokana mikata mibovu ambayo serikali imekuwa ikiingia.

Ally alisema takribani kipindi cha miaka 20, ofisi hiyo imekuwa ikingia mikataba mbalimbali ambayo badala ya kuwa na tija kwa taifa imekuwa ikisababisha hasara za mabilioni ya fedha. “Werema amerithi ofisi inayonuka rushwa, kwa kipindi kifupi tangu akae katika ofisi hiyo, bado hatujaona juhudi zozote za kusafisha uchafu huu, na vizuri Werema mwenyewe anayajua vema haya kwasababu amekulia katika ofisi hiyo siyo mtu kutoka nje,” alieleza Ally. Alisema kupitia ofisi hiyo, kwa muda huo wa miaka 20 sekta ya madini na nishati kupitia mikataba mibovu inayobarikiwa na ofisi hiyo, imeongoza kwa kulisababishia taifa hasara kubwa.

Ally alitaja baadhi ya mikataba hiyo kuwa ni pamoja na ule wa Kaumpuni ya kufua umeme ya IPTL, Richmond, ununuzi wa Rada na Dowans. “Sasa suala siyo kuangalia kama tulipe ama tusilipe hizo fedha kwa Dowans, ikumbukwe katika nafasi yake ofisi ya mwanasheria mkuu lazima nao walihusika kutoa ushauri wakati wa kesi hii, kwa hiyo jambo la msingi kufahamu Tanzania hatujawahi kuwa na mwanasheria wa serikali anayeweza kusimamia maslahi ya umma,” alisema Ally.

Mbunge wa Kigoma Kaskazini kupitia Chadema, Zitto Kabwe yeye alisema wanasiasa lazima wawajibike katika mjadala wa Kampuni ya Dowans kwa kuwa siasa ziliingia kuanzia kutolewa kwa zabuni hadi kuvunjwa kwa mkataba. Zitto alisema kuwa anaisubiri hoja ya Kafulila kuhusu umeme ili aweze kuzungumzia Dowans na kutoa maoni yake. "Suala la msingi hapa ni kujua je ni sawa kulipa Dowans? Bunge lilisema mkataba si halali, mahakama imesemaje kuhusu hilo? Bunge lilisema kampuni ni feki, mahakama imesemaje? Alihoji Zitto.

Alisema kuwa Sh 185 bilioni ni fedha nyingi sana kulipa bila kupata majibu hayo kwani fedha hizo zina uwezo wa kuweka lami kwenye barabara ya kimometa 200 kama Manyoni-Tabora. "Sakata zima lilijaa siasa na ndo maana tuko hapa,"alisema Zitto.

Kauli ya Zitto inaungwa mkono na ile ya Mkurugenzi wa Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD), Dk Benson Bana amesema serikali ikate rufaa,ili kujiridhisha kama kweli kampuni ya Dowans inastahili kulipwa kiasi hicho cha fedha. "Hizi ni fedha za walipakodi, tusikurupuke kulipa kabla hatujajiridhisha bila kuwa na shaka kwamba kampuni ya Dowans inastahili kiasi hicho cha fedha," alisema.

Alisema inasikitisha kuona wananchi wanayumbishwa na viongozi wasiojua madhara ya maamuzi wanayoyachukua. "Baadhi walishangilia wakati mkataba wa Dowans na Tanesco ulipovunjwa, viongozi walitumia nafasi ya kuvunjwa kwa mkataba huo ili kukamilisha malengo yao ya kisiasa, sasa ni zamu ya kodi ya wananchi kulipa deni hilo," alisema.

Naye Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema Makao Makuu Erasto Tumbo alimshukia Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kueleza kuwa mjadala wa Dowas umefungwa kilichobaki kulipa deni hilo akihoji ana maslahi gani na kampuni hiyo. Alisema hoja iliyopombele ya Watanzania kwa sasa ni kujua nani mmiliki wa kampuni na pia kuona serikali inakata rufaa kama alivyowahi kubainishwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

“Huyu Warema ni nani hata atuambie Watanzaia mjadala huo umefungwa,ana maslahi gani na kampuni ya Dowans, naomba akae kimya awaache Watanzania wamjue mmiliki wa Kampuni hiyo inayotaka kuchota mali za Watanzania”alisema Tumbo.

Imeandaliwa na Fidelis Butahe, Hussein Issa, Boniface Meena, Fredy Azzah, Raymond Kaminyonge na Geofrey Nyang'oro

No comments:

Website counter