Wednesday, December 8, 2010

HAPA NDIPO NINAPOMKUBALI HUYU MZEE, SEMA BABA USIOGOPEE TUKO NYUMA YAKOO...

Sitta: Kuilipa Downs ni kuhujumu uchumi Send to a friend

ASEMA HIZO NI NJAMA ZA GENGE LINALOTAFUTA FEDHA ZA UCHAGUZI MKUU 2015
Na Mwandishi Wetu

WAZIRI mpya wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, ambaye ni mjumbe wa Baraza la Mawaziri, amesema hatua yoyote ya kulipa fidia ya Sh 185 bilioni kwa kampuni ya Dowans, ni kuhujumu uchumi wa nchi.

Sitta, ambaye aliongoza Bunge la Tisa lililotikisa nchi kwa kuibua kashfa za ufisadi, pia amesema kuna kila dalili za genge linalohujumu nchi kuandaa mpango wa kutafuta fedha kwa ajili ya uchaguzi wa 2015.

Sitta alikuwa akitoa maoni yake baada ya hukumu ya Mahakama ya Kimataifa ya Usuhishi wa Kibiashara (ICC) iliyolitaka Shirika la Umeme (Tanesco) kuilipa Dowans Sh185 bilioni kutokana na kuvunja mkataba bila ya kufuata taratibu.

Tanesco ilivunja mkataba huo wa kuzalisha umeme mwaka 2008, ikiwa ni mwaka mmoja kabla ya kuisha, ikieleza kuwa mkataba huo ulikiuka Sheria ya Manunuzi ya Umma. Tanesco imesema itazungumzia suala hilo baada ya hukumu hiyo kusajiliwa nchini.

Hukumu hiyo imeamsha mjadala mkubwa uliokuwa umepoa kuhusu kampuni ya Dowans ambayo ilirithi mkataba uliobainika kuwa wa kifisadi wa Richmond Development LLC ambayo ilitakiwa izalishe umeme wa dharura wakati kulipotokea tatizo kubwa la umeme mwaka 2006.
Jana Sitta alizidi kuukoleza mjadala huo aliposema: "Kuna kila dalili ya genge la watu wenye fedha chafu kujaribu kuandaa mpango wa kuihujumu nchi."
"Hakuna uhalali wowote wa kuilipa Dowans kiasi hicho cha fedha, si haki hata kidogo.
"Kuilipa Dowans Sh185 bilioni ni kuhujumu uchumi wa nchi, na kuna kila dalili ni genge lilelile ambalo sasa linatafuta fedha kwa ajili ya uchaguzi wa 2015."
Sitta, ambaye aliweka bayana dhamira yake ya kuendelea kupambana na ufisadi mara baada ya kuapishwa kuwa waziri, aliendelea kusema: "Ni genge ambalo halina huruma na nchi na umasikini wa Watanzania... na kama likiachwa lijiimarishe, Watanzania wasubiri matatizo makubwa zaidi huko mbele.
"Genge hili limekuwa likiwafanya Watanzania kuwa ni wajinga wasioweza kufikiri. Ni kwa sababu limeshika nchi, linafikiri siku zote litafanya mambo ya hovyo na kuangaliwa... sijui linawatafuta nini Watanzania wazalendo?"
Mbunge huyo wa Urambo Mashariki ambaye wakati akiwa spika Bunge lilijadili kwa kina kashfa ya Richmond iliyokuwa na matokeo ya kihistoria baada ya Edward Lowassa kulazimika kuachia uwaziri mkuu na kufuatiwa na mawaziri wengine wawili, alisema kinachofanyika sasa ni genge hilo kujiandalia mazingira ya kujikusanyia mabilioni ya fedha chafu za uchaguzi wa 2015.
Pamoja na Tanesco kuvunja mkataba na Dowans mwaka 2008, shirika hilo la umma liliibuka na mapendekezo ya kununua genereta za kampuni hiyo zinazoendeshwa kwa gesi, mapendekezo ambayo Bunge la Sitta liliyakataa kwa maelezo kuwa yanakiuka Sheria ya Manunuzi ya Umma.
Msimamo huo wa Bunge ulimfanya mkurugenzi wa zamani wa Tanesco, Dk Idris Rashid kukubali kwa shingo upande akilaumu wanasiasa kwa kukwamisha masuala ya kitaalamu na kunawa mikono kwamba asilaumiwe kwa matatizo ya baadaye ya umeme.


Wakati nchi ikiwa imeingia kwenye tatizo jingine kubwa la umeme linalokaribiana na la mwaka 2006, ICC ilitoa hukumu ambayo imeamsha mjadala huo na Sitta alisema jana kuwa Tanesco isilaumiwe kwa uamuzi huo akielekeza lawama zake kwa genge hilo ambalo hakutaja walio ndani.
"Nitashiriki kikamilifu kuhakikisha maslahi ya taifa yanalindwa na hakuna mianya yoyote ambayo genge hili inaweza kuitumia kuhujumu nchi," alisema Sitta, ambaye ni mmoja wa wanasiasa wazoefu walio kwenye baraza jipya la mawaziri.


"Hili nataka uninukuu vizuri, kwamba sasa ni dhahiri kuna mkono wa ambao kila dalili unaonyesha ni genge linalotaka kufanya hujuma. Linachotaka kufanya ni mchezo mchafu ambao sisi serikalini tutajitahidi kuuzuia."
Alifafanua kwamba watu hawapaswi kuitwisha mzigo Tanesco kwani uamuzi uliangal;ia kwa kina maslahi ya taifa kuliko baadhi wanavyojaribu kupotosha.


Sitta alisema huu ni wakati wa kuhakikisha genge hilo halifanyi hujuma zake kwa nchi.
Sitta pia alidai kuwa baadhi ya watuhumiwa wa ufisadi nchini wamekuwa wakikwepa kufungua kesi zao kwenye mahakama za ndani kwa hofu ya kuumbuka.
Dowans ilifungua kesi hiyo kwenye mahakama hiyo ya ICC ambayo makao yake makuu yako Paris, Ufaransa.


No comments:

Website counter