|  
  Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto KabweMBUNGE  wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe ambaye jana aliruhusiwa kutoka katika  Hospitali ya Aga Khan ya jijini Dar es Salaam alikolazwa kwa matibabu ya  tumbo amedai kuwa matatizo hayo aliyapata baada ya kula chakula chenye  sumu.
 “Namshukuru Mungu naendelea vizuri na nimesharuhusiwa kutoka  hospitali, madaktari wameniambia ilikuwa food poisoning (chakula chenye  sumu),” alisema Zitto.
 Zitto ambaye hakuweza kueleza chakula  hicho alikuwa wapi na kina sumu ya aina gani, alisema kuwa baada ya  kugundua tatizo hilo, madaktari walimtaka kuwa makini na vyakula  anavyokula.
 
 “Sumu gani nimekula na ni wapi, mimi nadhani sio  story (habari). Cha msingi kwa sasa naendelea vizuri na nimetakiwa kuwa  makini na vyakula ninavyokula,” alisema Zitto.
 
 Hata hivyo, kauli  hiyo ya Zitto inapingana na madaktari wake waliosema kuwa mbunge huyo  kupitia tiketi ya Chadema, alikuwa anasumbuliwa na mchafuko wa kawaida  wa tumbo.
 
 “Alikuwa anasumbuliwa na Gastro enteritis (mchafuko wa  tumbo), tatizo hili linaweza kusababishwa na bacteria, virusi katika  chakula, au kama chakula hakijapikwa vizuri,” alisema Dk Mustafa  Bapumia.
 
 Zitto alilazwa hospitalini hapo tangu Disemba 9 mwaka  huu saa 3:00 usiku, baada ya kutoka kwenye mkutano wa ndani wa chama  chake uliofanyika Bagamoyo mkoani Pwani ambako alivuliwa cheo cha Naibu  Kiongozi wa Kambi ya upinzani bungeni.
 
 Kuhusu hatua ya chama  hicho kumvua Zitto wadhifa wake wa unaibu kiongozi wa upinzani bungeni,  alisema kwa sasa bado hawezi kuzungumzia suala hilo kwa sababu hajapata  taarifa rasmi kutoka chama chake mbali na kusoma suala hilo kwenye  vyombo vya habari.
 
 Hata hivyo, alieleza hakuwahi kuomba kupewa  wadhifa huo, kwa hiyo endapo watu waliomwona anafaa kufanya kazi na  kumpa wadhifa huo, wakiamua kumnyang’anya siyo tatizo kubwa kwake.
 
 “Kwa  sasa nadhani suala la afya yangu ndiyo muhimu zaidi. Ngoja kwanza  nitoke hapa na afya yangu iimarike na kama kutakuwa kuna sababu ya mimi  kuzungumza nitazungumza,” alisema Zitto:
 
 “Lakini ikumbukwe kuwa  mimi sikuwahi kuomba wadhifa huu…, kwa hiyo kama watu walionipa wameamua  kunibadilishia, mimi sidhani kama kuna tatizo.”
 
 Mwenyekiti wa  chama hicho, Freeman Mbowe aliupolizwa na Mwananchi Jumapili juu ya  Zitto kuvuliwa uongozi bungeni alisema kuwa chama kitatoa taarifa  baadaye.
 
 Katika hatua nyingine Mbunge wa Mpanda Mjini, Said Amur  Arfi aliyekuwa amelazwa katika Hospitali ya Aga Khan ya jijini Dar es  Salaam, amesafirishwa kwenda India kwa matibabu zaidi.
 
 Arfi  aliliambia Mwananchi Jumapili kuwa madaktari waliokuwa wakimtibu  wamemwambia kuwa mfuko wake wa nyongo una mawe hivyo anahitaji kufanyiwa  upasuaji.
 
 “Nilikuja hapa kwa sababu nilikuwa nasumbuliwa na  maumivu makali ya tumbo, nilitoka Mpanda Disemba 2, mwaka huu kuja  kwenye semina lakini kutokana na maumivu ya tumbo nilienda Hospitali ya  Regency na baada ya kupigwa ultrasound nilielezwa kuwa nina tatizo la  uvimbe kwenye maini,” alisema Arfi.
 
 Alisema alivyokwenda katika  Hospitali ya  Aga Khan alielezwa kuwa ana tatizo jingine la mawe kwenye  mfuko wa nyongo na kuwa inabidi afanyiwe upasuaji.
 
 “Naishukuru serikali kupitia ofisi ya Bunge kunipeleka India kwa matitabu zaidi,” alisema Arfi.
 
 Hata  hivyo, alisema bado hajaelezwa hospitali anayokwenda kutibiwa na kuwa,  taarifa zote hizo anazo muuguzi wa serikali atakayesafiri naye.
 Wakati  huohuo, Mtangazaji wa Televisheni ya Channel Ten, Cyprian Musiba,  anadaiwa kuwekewa sumu kwenye chakula na kufanya alazwe hospitalini kwa  matibabu.
 
 Musiba alilazwa katika kituo cha Afya cha Ebrahim Haji kilichopo jijini Dar es Salaam juzi mchana akiwa hajitambui.
 
 Mmoja  wa madaktari wa hospitali hiyo, Dk Ramadhani Ali aliliambia Mwananchi  Jumapili kuwa Musiba alifikishwa katika hospitali hiyo akiwa  anasumbuliwa na tumbo lakini, baada ya kupata matibabu, afya yake  iliimarika na jana mchana aliruhusiwa kutoka hospitalini.
 
 “Anaendelea vizuri kwa kweli na amesharuhusiwa” alisema Dk Ali huku akisita kueleza tatizo la lililokuwa linamsumbua Musiba.
 
 Mke  wa Musiba ambaye hakujitambulisha alisema kuwa kabla ya Musiba  kuruhusiwa  mmoja wa madaktari wa HospitaliI hiyo waliwaeleza kuwa  Musiba alikula sumu iliyokuwa katika chakula.
 
 “Tumeruhusiwa muda  si mrefu ila daktari amesema Musiba alijisikia vibaya kwa kuwa alikuwa  amekula sumu iliyokuwa katika chakula,”alisema  mke wa Musiba.
 
 Musiba  ambaye mara nyingi hutangaza habari za michezo na burudani aliliambia  Mwananchi Jumapili  kuwa juzi hali yake ilikuwa mbaya  na kuongeza kuwa  alipelekwa katika hospitali hiyo kwa ajili ya matibabu.
 
 “Hali  yangu ilikuwa mbaya sana nilikuwa wa kufa tu ndugu yangu, ila namshukuru  mungu naendelea vizuri, ila daktari hapa hospitali amenieleza kuwa  nilikula sum,” alisema Musiba.
 
 Habari zaidi zilidai kuwa Musiba  alianza kupata matatizo ya tumbo saa kadhaa baada ya kula chakula katika  hoteli moja iliyopo  karibu na ofisi za Channel Ten.
 
 | 
No comments:
Post a Comment