Thursday, September 15, 2011

KWANI NI KOSA KWA HUYU BWANA KUJICHONGEA 'MSALABA' WAKE JAMANI...



Nilipoamua kuitoa habari hii ya Gilbert Paul na Msalaba wake hapa Bloguni sikutegemea kuwa ningeweza kutumiwa ujumbe kutoka kwa wadau mbalimbali na wengi walimpongeza sana msanii huyu kwa kuanzisha mada kuhusu kifo lakini kwa nia ya ubunifu kabisa ya kujichongea msalaba wake. Kama msomaji aliyesema hilo ni jambo jema kwani hata dini yake ya Kiislamu inaunga mkono dhana ya kujiweka tayari na kifo.

Lakini kuna msomaji wangu mmoja aliandika barua pepe ndefu na nimeona bora leo nimpe nafasi kwenye Blogu hii ili naye asomwe na wananchi wenzangu ili kuendeleza mjadala.

“Nimeguswa sana na makala yako ya leo ya kwa habari ya bwana Gilbert Paul. Hongera sana kwa jicho lako kuona hilo na kutufikishia wadau kujua hisia za watu wengine. Tumezoea kuona habari za wasanii, nyingi zikiwa za watu wa DAR ES SALAAM kwani ndiyo imani ya wengi kuwa DAR ES SALAAM ndio kwenye kila kitu kumbe hata mikoani kuna wasanii wabunifu zaidi hata kuliko baadhi ya waliopo DAR ES SALAAM isipokuwa hawapati nafasi ya kuonyesha uwezo wao kwa vyombo vya habari ambavyo karibuni vyote vipo huko DAR ES SALAAM.

“Kwa kuwa bwana Gilbert ni msanii katika fani ya uchoraji aliamua kujitangaza katika style (mtindo) yake ya kipekee ambayo ilimgusa kila mmoja, na pengine huyu bwana hakuwa na mawazo kabisa ya kujitabiria kifo chake isipokuwa jamii inayomzunguka (lakini hiyo ) ilikuwa ndio iliyotafsiri ya hilo.

“Sisi waafrika katika mila zetu nyingi kuna baadhi ya vitu tumewekewa imani vikijadiliwa au kuwekwa katika maandishi basi inaonekana kuwa ni uchuro kwa mtu husika, alichokifanya Gilbert hakina tofauti na mzazi aliyeamua kuandika wosia, kwetu huwa ni suala gumu sana kwa mzazi kufanya hivyo na akifanya hivyo huwa ni siri kubwa na ikigundilika kwa watoto basi mzazi huufuta mara moja. Hii hutokea mara nyingi.

“Pia bila kujali imani yako watu wanatabia ya kupenda kuyafanya na kuyatenda yale tu yanayofurahisha nafsi zao, mfano dini karibu zote zinakataza zinaa, lakini kuna baadhi ya watu wanafanya zinaa kiasi kwamba watu wanamzunguka walijua hilo na halipingiki kuwa zinaa ni chanzo kikuu cha ugonjwa wa ukimwi.

Je nikuulize Bw. Ben umesha wahi kuona jamii inamkimbia au kumtenga mtu wanayemfahamu kuwa anazini sana? Tena akiwa mwenye kipato kila mtu atataka awe karibu yake. AU makahaba waliojaa katika mabaa na majumba ya starehe mbona hawakimbiwi ndio kwanza wanakimbiliwa mpaka wakianza kuugua ndio kila mmoja anaanza kujiweka pembeni.

Maana yangu katika "paragraph" hii ni kuwa bw. Gilbert amewasilisha hisia zake katika jamii kulingana na kazi yake, lakini jamii imemsukuma katika mahali ambapo sipo. kwa wale waliomnyima kazi kwa kuona msalaba wana uhakika gani kwa mfano kuwapelekea kazi wale ambao yawezekana ni wazinifu wa kupindukia ambao maisha yao yapo hatarini zaidi ya Tangazo la bw. Gilbert?

Nakutakia kazi njema na BLOGU yako na uendelee kutuletea taarifa nzuri zenye mafunzo katika jamii kama habari hii ya bw. Gilbrt Paul.


No comments:

Website counter