|  Mchungaji  Ambilikile Mwasapile akiweka dawa katika vikombe ambavyo husambazwa  kwenye magari kwa wagonjwa na wananchi walifika upata tiba katika kijiji  cha Samunge, Loliondo, mkoani Arusha. Picha na Mussa JumaWAKATI  dawa aliyoigundua Mchungaji Ambilikile  Mwasapile ikionekana kuwavuta  watu karibu nchi nzima kutaka kuinywa, baadhi ya wakazi wa Arusha  wameamua kwenda maporini kusaka dawa hiyo.
 Taarifa ambazo pia  zimemfikia mchungaji huyo mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri  Tanzania (KKKT), zimeeleza kuwa watu hao tayari wamevamia pori la mlima  Sonjo kuchimba dawa anayotumia kutibu.Hata hivyo, Mchungaji Mwasapile  alisema haitawasaidia kwa vyovyote kwa sababu ni yeye pekee aliyepewa  uwezo na Mungu ili awaponye watu.
 Hata hivyo, Mchungaji  Mwasapile, ameiomba Serikali kuingilia kati kwa kuwadhibiti watu hao,  aliowaita kuwa ni matapeli ambao tayari wamevamia pori hilo kwa sababu  watasababishawatasababisha watu wengine kuikosa kwa vile uchimbaji  utakuwa ni wa vurugu na pia utasababisha uharibifu wa mazingira.
 
 Akizungumza  na waandishi wa habari, mchungaji huyo alisema watu hao, wamekuwa  wakiwatumia baadhi ya vijana wa kijiji cha Samunge ambao wanaujua mti wa  Mugariga, au Mungamuryogo na wameanza kuchimba mizizi na kusafirisha  nje ya kijiji hicho.
 
 "Naomba nitoe angalizo, hii dawa ni mimi  pekee ndiye Mungu ameniotesha kuitoa na inakwenda pamoja na maombi sasa  hawa wanachimba mizizi na kwenda kutengeneza haitawasaidia ni utapeli,"  alisema Mchungaji Mwasapile.
 
 Mchungaji huyo aliiendelea kuiomba  Serikali kukarabati miundombinu ya kufika katika kijiji cha Samunge kwa  sababu sasa mvua zimeanza kunyesha na kwamba siku si nyingi barabara za  kumfikia zitakuwa hazipitiki.
 Kutokana na ubovu wa barabara hiyo,  gari lililokuwa limembeba Waziri Mkuu Mstaafu lilikwama juzi jirani tu  na kwa mchungaji huyo sambamba na magari mengine kadhaa.
 
 Kukwama  kwa magari hayo, kulitokana na mvua ambazo zimeanza kunyesha na kuharibu  barabara ya kwenda katika kijiji hicho, inayotokea eneo la Kigongoni  Mto wa Mbu, kupitia kata za Selela, Engaruka na Ngaresero.
 Magari  mengi yalikuwa yameharibika na kukwama kati kati ya miti juzi, hali  ambayo inatishia usalama wa barabara hiyo ambayo ni ya vumbi.
 
 Akizungumzia  barabara hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Elias Wawa Lali, aliwataka  madereva kuwa makini ili kuzuia mfululizo wa ajali.
 
 Katika hatua  nyingine, Mchungaji Mwasapile alirudia tena onyo lake la kuwataka watu  kuacha kuwapeleka kwake wagonjwa waliotoroshwa hospitali huku wengine  wakiwa na chupa za kuongezewa maji mwilini.
 
 "Wanakuja huku wakiwa  na Dripu za maji. Sasa hapa sio hospitali ya rufani. Wagonjwa waletwe  hapa kwa tahadhari kubwa kwanza barabara zetu sio nzuri," alisema  Mwasapile.
 Idadi ya magari na watu toka ndani na nje ya nchi  inaongezeka katika kijiji hicho na sasa kupata dawa mgonjwa inachukuwa  kati ya siku mbili hadi tatu.
 
 Mwandishi wa habari hizi juzi  alishuhudia wagonjwa toka nchi za Kenya, Zambia, Malawi, Uganda na  Afrika Kusini wakiwa wamepanga foleni ya kupata dawa.
 
 Madaktari wa Moshi
 Kutoka  Moshi, madaktari mbalimbali wameitaka Serikali kuandaa kongamano la  wanasayansi kujadili tiba inayotolewa na Mchungaji Mwasapile, ikiwamo  kutolewa kwa ripoti za kisayansi za wagonjwa waliopona. Wakizungumza na  Mwananchi, madaktari hao wamedai kisayansi haiwezekani kupima dawa  inayotokana na imani ya dini, lakini ni vyema wakapatikana wagonjwa  wanaodai kupona wakiwa na kumbukumbu za matibabu ya siku za nyuma.
 
 Mmoja  wa madaktari bingwa, Profesa Waitoki Nkya, ambaye sasa amestaafu  serikalini alisema Taifa bado liko gizani kuhusu ukweli wa nguvu ya dawa  hiyo katika kutibu magonjwa sugu ukiwamo Ukimwi, kisukari na saratani.
 
 “Binafsi  siamini katika jambo hilo lakini, naishangaa Serikali na vyombo vyake  kwamba  kweli vimeshindwa kutuambia mgonjwa X wa Ukimwi alikuwa na CD4  200, baada ya kunywa zimeongezeka hadi 1,000?” alijoji.
 
 Profesa  Nkya ambaye aliwahi kufanya kazi Hospitali ya Rufaa ya KCMC na  kuhamishiwa Hospitali ya Rufaa ya Mbeya kabla ya kustaafu, alisema taifa  linaweza kuondokana na giza hilo kwa wataalamu kuthibitisha nguvu ya  dawa hiyo.
 
 Profesa Nkya alisema Tanzania kama Taifa haliwezi  kuruhusu watu waliokunywa dawa hiyo kujisemea wenyewe kuwa wamepona  wakati hakuna hata mmoja anayethubutu kutoa vipimo vya awali na vya sasa  kuthibitisha amepona.
 
 Hata hivyo, daktari mmoja ambaye ni  mratibu wa Ukimwi kwa zaidi ya miaka 10 sasa, alisema katika suala la  Ukimwi bado hajathibitisha nguvu ya dawa hiyo isipokuwa kwa magonjwa ya  kisukari na shinikizo la damu (BP).
 
 “Kwa kisukari na BP naweza  kusema kuna mafanikio kidogo kwa sababu kuna wagonjwa wetu wa kisukari  walikuwa katika hatua ya kudungwa sindano kila siku lakini, sasa wana  wiki hawajachoma sindano na wako vizuri,” alidai.
 
 Daktari  mwandamizi katika Hospitali ya Mkoa Kilimanjaro ya Mawenzi, Dk Issa  Mbaga, ambaye alisema anatoa maoni binafsi na sio ya Taasisi yake,  alisema tatizo ni waliokunywa dawa kutopima upya kuthibitisha kupona.
 “Unajua  ni vigumu kupima jambo kiimani kama ilivyo kunywa dawa ya Babu kule  Loliondo lakini, hawa waliorudi na kutuambia wanaendelea vizuri kwa nini  wasipime upya wakatupa ripoti?” alihoji Dk. Issa.
 
 Wazidi kwenda Loliondo
 Wakati  huo huo, kitimutimu cha wananchi kutaka kwenda huko kimesikika karibu  kila mkoa hapa nchini ila tatizo kubwa ni gharama za usafiri pamoja na  chakula.Katika Manispaa ya Shinyanga watu wengi wamejitokeza kwenda  kujiandikisha ili waende Loliondo baada ya kupata taarifa kuwa Mbunge  wao,  Steven Masele amekusudia kuwagharimia usafiri.
 
 Wananchi hao  walikusanyika jana kwenye ofsi ya mbunge kujiandikisha na awamu ya  kwanza ya kundi la watu hao ilitarajia kuondoaka jana.Akizungumza na  Mwananchi kwa njia ya simu mbunge huyo alisema kuwa amegharimia safari  hiyo bila kujali wanaoenda ni wagonjwa au la.
 
 Hata hivyo, alisema  wale wenye uwezo washiriki watapaswa kuchangia kiasi kidogo cha fedha  ili kutoa nafasi ya watu wengi wanaomiminika katika ofisi yake ili  kujiandikisha kwa safari.
 
 Mwanza nako
 Jijini  Mwanza nako watu wengi wamesikika wakitaka kupata tiba hiyo miongoni  mwao ni wafanyakazi Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza ambao tayari  wameanza kuchangishana ili kugharimia safari.
 
 Habari  zilizopatikana toka ofisi ya mkuu wa mkoa huo na kuthibitishwa na Ofisa  Usafirishaji wa Mkoa, William James zilieleza kwamba wafanyakazi hao  wamekusudia kwenda kabla ya kufika mwishoni mwa mwezi huu.
 
 James  alisema hadi jana wafanyakazi 26 walikuwa wamejiorodhesha kwenda na kila  mmoja tayari amelipa Sh80,000.Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Abbasi Kandoro,  alielezea kuwa hahusiki katika mpango huo kwa sababu hiyo ni safari  binafsi.“Hii siyo suala la ofisi ni wafanyakazi binafsi, ndiyo maana  uliponiuliza nilishangaa na kwa vile mimi sikuwepo nilikuwa sijui  lolote," alisema Kandoro.
 
 Morogoro nao wamo
 Kutoka  mkoani Morogoro, inaripotiwa kuwa Watu  Wanaoishi na Virusi vya Ukimwi  (Wavumo) wamemwomba mbunge wa jimbo la Morogoro Mjini, Aziz Abood   kuwapa msaada wa kuweza kufika Loliondo ili kupata dawa ya  'Babu'.Akizungumza na waandishi wa habari jana katika ofisi za Wavumo,  katibu wa  kikundihicho, Said Shija alisema kuwa wao nao wamehamasika na  dawa hiyo.
 
 Alisema kuwa wao wana imani na dawa hiyo na kwamba  kinachowashinda hadi sasa kufika huko Loliondo ni kwamba hawana uwezo na  kumudu gharama za usafiri.
 
 Askofu Kakobe
 Jijini  Dar es Salaam,  Askofu  wa Kanisa la Full Gospel Fellowship,  Zacharia   Kakobe, ameendelea kutoa maneno ya shutuma dhidi ya mchungaji  Mwasapile.
 
 Hii ni baada ya Mwasapile kusema kwamba anawakaribisha  ili kunywa dawa hiyo licha ya kumdharau pamoja na tiba anayoitoa.  Kakobe amerusha kombora lingine akidai haendi ng’o na yeye sio nyasi  zinazotikiswa na upepo kama watu wengine wanaokwenda huko.
 
 Mwasapile  maarufu kwa jina la ‘Babu’ aliwajibu viongozi hao waliomtuhumu kuwa  tiba anayoitoa ni ya nguvu za giza,  akisema kuwa waliotoa tuhuma hizo  wana mtazamo wa kifedha zaidi na sio imani.
 
 Akizungumza na gazeti  hili jana kwa simu, Askofu Kakobe alisema kwanza anawahurumia  wanaoendelea kwenda huko kwa sababu tayari wameshatekwa na huduma hiyo  ya 'kitapeli.'
 
 “Siwezi kwenda kunywa dawa hata kidogo, kwa sababu  mimi sio nyasi zinazotikiswa na upepo kama wengine waliokwenda huko,”  alisema Askofu Kakobe.
 
 Ajali Loliondo
 Kwa upande mwingine, ajali za magari yanayoenda, au kutoka kwa 'Babu' nazo zinaendelea kuongezeka.
 Jumatano  iliyopita mtu mmoja alikufa na wengine watano kujeruhiwa baada  ya gari  lililokuwa njiani kwenda Loliondo kupasuka tairi na kupinduka eneo la  Makuyuni, wilayani Monduli.
 
 Ajali hiyo inafanya idadi ya watu  waliokufa tokea msururu wa watu toka pembe zote za nchi walipoanza  kumimika katika kijiji cha Samunge, Wilayani Ngorongoro kufiki saba.
 
 Kaimu  Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Akili Mpwapwa alithibitisha kutokea  kwa ajali hiyo. Alisema ajali hiyo ilitokea saa nane mchana kufuatia  kupasuka kwa gurudumu la nyuma la gari hilo, kisha kupinduka.
 Alimtaja aliyefariki dunia kuwa ni Fatuma Badru (34), mkazi wa Soweto mjini Moshi.
 
 Aliwataja majeruhi kuwa ni Ruth Lyimo, Mary Sembugao na Salma Badru na mmoja aliyefahamika kwa jina moja la Omary.
 
 Habari  hii imeandikwa na Mussa Juma-Loliondo,  Daniel Mjema-Moshi, Suzy  Butondo-Shinyanga, Frederick Katulanda-Mwanza, Filbert Rweyemamu-Arusha,  Lilian Lucas-Morogoro na Elizabeth Suleyman - Dar.
 
 | 
No comments:
Post a Comment