Wednesday, February 16, 2011

KAMA MKATABA HAUELEWEKI SI 'MUITAIFISHE' HIYO MITAMBO JAMANI, TUMECHOKAA!


Mitambo ya Kuzalisha umeme wa dharura ya Dowans iliyopo Tanesco Ubungo Jijini Dar es salaam.


MITAMBO ya kuzalisha umeme wa dharura ya Dowans iliyoibua mjadala mpana katika jamii kutokana na utata wa mkataba wake, huenda ikawashwa wakati wowote kwa malengo ya kupunguza tatizo la mgawo wa umeme linaloendelea nchini.

Habari zilizopatikana jana mjini Dodoma na kuthibitishwa na baadhi ya wabunge waliohudhuria kikao cha Kamati ya Nishati na Madini walisema kuwa hoja ya kuwashwa kwa mitambo hiyo ilijadiliwa kwa lengo la kupunguza makali ya umeme nchini.

Chanzo chetu cha habari kilisema kwamba wajumbe wa kamati hiyo walikuwa wakijadili ama waitaifishe mitambo hiyo au waingie mkataba wa dharura ili ianze kutoa umeme kwa siku mbili zijazo.

"Suala lililozua mvutano baina ya wabunge ni ama kutaifisha au kuwapo mkataba wa dharura na kampuni inayomiliki mitambo hiyo,"alisema mbunge mmoja aliyekuwapo katika kikao cha kamati hiyo.

Vyanzo hivyo vya habari vilieleza kuwa mpaka jana usiku kikao kilikuwa kikielendea na kwamba baada ya kumaliza kikao hicho wangeshauriana na Spika wa Bunge kueleza msimamo wao.

Alipoulizwa Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, January Makamba kilichokuwa kikijadiliwa ndani ya kikao, alisema : " Kikao bado kinaendelea. Tutashauriana na Spika baada ya hapa. Tunatarajia kufanya maamuzi yenye maslahi ya kwa nchi nzima."

Awali jana asubuhi wakizungumza katika kipindi cha Jambo Tanzania cha TBC1 , Makamba, Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, John Mnyika walipendekeza yafanyike maamuzi magumu ili kuwezesha mitambo ya Dowans kuwashwa ili kupunguza makali ya mgao.

Kwa mujibu wa Makamba, mitambo ya Dowans inazalisha MW 120 na itasaidia kupunguza makali ya mgao kwa asilimia 60 mpaka 70. Wote walitambua uwepo wa suala la Dowans mahakamani.

Hata hivyo, Mnyika alipendekeza sheria ya uhujumu uchumi itumike katka suala la Dowans huku akisema kuwa hawezi kwenda ndani zaidi.

Mniyka alimaanisha kuwa mitambo ya Dowans inapaswa kutaifishwa kwa sababu ya ukweli kuwa mkataba wa Dowans/Richmond ni wa kitapeli na huwezi kuwa na mgawo wakati mitambo iko pale imezimwa.

Wakati huo huo, Makamba alipendekeza kuwa usainiwe mkataba wa muda mfupi wa miezi mitatu na hao wenye mitambo ili kuiwezeshwa kuwashwa. Alipendekeza uangaliwe utaratibu ambao hautaathiri kesi iliyopo Mahakamani.

Spika Makinda azuia Bunge kujadili umeme

SPIKA wa Bunge, Anne Makinda jana alizuia kufanyika kwa mjadala wa umeme bungeni baada ya mbunge wa Ubungo na Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, John Mnyika kutoa hoja ya dharura.

Mnyika alitoa hoja ya kutaka kuahirishwa kwa shughuli za Bunge na kujadili suala la dharura akinukuu kifungu cha 47(1) na 55 (3) vya Kanuni za Bunge vinayoruhusu mbunge kutoa hoja ya kujadili jambo la dharura na muhimu kwa jamii baada ya kipindi cha maswali na majibu.

Kifungu hicho kinasema: "Baada ya muda wa maswali kwisha, Mbunge yeyote anaweza kutoa hoja kuwa shughuli za Bunge kama zilivyoonyeshwa kwenye orodha ya shughuli, ziahirishwe ili Bunge lijadili jambo halisi la dharura na muhimu kwa umma."

Akitoa hoja hiyo, Mnyika alisema; " Hoja ya dharura." kauli hiyo ilipokelewa kwa swali kutoka kwa Spika Makinda aliyeuliza: "Dharura gani tena, usianze kwa hotuba."

Ndipo Mnyika alipotoa maelezo ya hoja yake ya dharura ambapo hata hivyo, Spika Makinda aliipangua na kuizima akitoa sababu za kutoikubali.

"Kwanza tusubiri, kamati hii ndio kwanza imeanza kazi, wamefanya kiako chao kimoja, juzi walienda kuangalia Bwawa la Mtera, wamepanga kukutana Dar es Salaam, tusubiri," alisema Makinda akimuuliza katibu wa shughuli za Bunge kuashiria waendelee na shughuli nyingine.

Hata hivyo, jana mchana Kamati ya Nishati na Madini jana ilikutana kwa dharura kujadili suala hilo huku Mwenyekiti wake akiahidi kukutana na wanahabari, lakini alishindwa kueleza kuwa walikuwa wakipumzika kabla ya kuendelea tena na kikao na kuahidi kutoa taarifa kesho Alhamisi.

Hatua za kuzuia mgawo

Wakati huohuo, Serikali imetolea tamko tatizo la mgawo wa umeme nchini na kutaja hatua sita za dharura ilizochukua katika kukabiliana na tatizo hilo sugu.

Akizungumza bungeni jana, Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja alitaja utekelezaji wa miradi ya umeme katika kipindi kifupi na cha kati kuwa moja ya hatua hizo zilizochukuliwa kumaliza tatizo hilo.

Waziri Ngeleja alitoa tamko hilo baada ya Spika wa Bunge, Anne Makinda, kumtaka afanye hivyo ili kumaliza kiu ya wabunge wa upinzani walioitaka Serikali itolee kauli suala hilo ili wananchi wajue hatima yake.

Februari 11 mwaka huu Kiongozi wa Kambi ya Upinzani bungeni, Freeman Mbowe katika swali la nyongeza, alimtaka Waziri Ngeleja kutolea kauli tatizo la umeme, lakini Spika Makinda aliizima hoja hiyo akisema haingekuwa rahisi kwa Waziri huyo kuzungumzia suala hilo muhimu katika kipindi cha maswali ya papo kwa hapo.

Na jana baada ya kupata fursa ya kuzungumzia tatizo hilo la mgawo wa umeme Ngeleja alisema Serikali kwa kushirikiana na Tanesco imechukua hatua sita tofauti.

Ataja hatua hizo za dharura kuwa ni pamoja na kuhakikisha fedha za kununulia mafuta ya kuendeshea kituo cha kuzalisha umeme cha IPTL zinaendelea kupatikana kwa wakati ili kizalishe kiwango cha Megawati 80 ambacho ni cha juu.

Pia kuharakisha mchakato wa kukodi mitambo ya dharura yenye uwezo wa kuzalisha zaidi ya megawati 260 endapo mvua za kutosha hazitanyesha kuwezesha ongezeko la umeme
unaotokana na maji na kutekeleza mpango wa kupanua miundombinu ya kusafuisha na kusafirisha gesi asilia kutoka visima vya Songosongo hadi Dar es Salaam.

Nyingine ni kuhakikisha miradi ya kudumu ya kuzalisha umeme ya Megawati 100 itakayofungwa Ubungo, Dar es Salaam kwa kutumia gesi asilia na mitambo ya megawati 60 itakayofungwa Mwanza kutumia mafuta mazito inakamilishwa kama ilivyopangwa Desemba 2011 na Januari 2012.

Ngeleja alitaja hatua nyingine kuwa ni kuendelea kutekeleza miradi ya kupunguza upotevu wa umeme kutoka asilimia 21 ya sasa hadi asilimia 15 kati ya mwaka 2011 na 2015, pamoja na Tanesco kusimamia mgawo wa umeme kwa umakini zaidi na kuhakikisha upatikanaji wa umeme katika shughuli za uzalishaji, sehemu nyeti za huduma za jamii, ulinzi na usalama.

Alisema kuwa wizara yake kwa kushirikiana na Tanesco inaendelea kusimamia utekelezaji wa programu ya kuongeza uwezo wa kuzalisha umeme katika kipindi kifupi cha 2011 hadi 2015 ili kuepusha tatizo la mgawo wa umeme siku za usoni ambapo alitaja miradi tofauti saba.

No comments:

Website counter