Thursday, January 20, 2011

DAAH NAMZIMIA SANA MZEE HUYU KWA UJASIRI WAKE...


Send to a friend



WAZIRI wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, amekoleza moto wa sakata la kampuni ya kufua umeme wa dharura ya Dowans, akisema kamwe hawezi kufungwa mdomo kupinga malipo ya Sh94 bilioni kwa kampuni hiyo.Kauli ya Sitta imekuwa wakati kukiwa na taarifa kwamba waziri huyo pamoja na Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk Harrison Mwakyembe wamebanwa na Ikulu wakitakiwa wasizungumzie tena suala hilo.

Hata hivyo, akizungumza na baadhi ya vyombo vya habari jijini Dar es Salaam jana Sitta alisema, "Naomba wananchi wafahamu, siwezi kufungwa mdomo kuhusu kupinga malipo kwa kampuni ya kitapeli ya Dowans."

Sitta ambaye msimamo wake umeibua mjadala mzito nchini na hata ndani ya baraza la mawaziri, alisema hajawahi kutishwa wala kufungwa mdomo kuhusu msimamo wake.

Kauli hiyo ya Sitta imekuja siku moja tangu gazeti moja la kila siku kuripoti kwamba Rais Jakaya Kikwete amemfunga mdomo, uamuzi uliodaiwa kufikiwa juzi katika kikao cha Baraza la Mawaziri, kilichofanyika Ikulu, jijini Dar es Salaam.

Habari hizo zilidai kuwa Sitta na Dk Mwakyembe walikuwa na wakati mgumu kutetea hoja ya kutaka Serikali isiilipe Dowans na kwamba hata Rais alisema hafurahishwi na hukumu ya malipo hayo, hivyo kikao hicho kuwaamuru mawaziri hao kutozungumzia tena suala hilo hadharani.

Lakini jana Sitta alisema: "Nitaendelea kupinga malipo ya Dowans. Sijawahi kuitwa popote wala na mtu yeyote na kuambiwa nisizungumze suala hilo, hivyo wananchi wasifikiri nimebadili msimamo".

Aliongeza: "Taarifa zinazosambaa ni za kupikwa tu, zisije zikawapotosha wananchi wakidhani nimewasaliti katika hili, narudia tena sijafungwa mdomo."

Mbunge huyo wa Urambo Mashariki ambaye aliliongoza Bunge la Tisa katika vita dhidi ya ufisadi, alifafanua kwamba si suala la Dowans tu bali ataendelea kupinga mambo yote machafu kuhusu nchi.

Aliweka bayana kwamba nchi inahitaji viongozi wenye uwezo wa kusimamia vema maslahi ya taifa bila hofu ili kulinda haki za wananchi na kuboresha maisha yao.

Sitta alinukuliwa akihoji kile kinachoitwa kukiuka dhana ya uwajibakaji wa pamoja na kuweka bayana, kama dhana hiyo ingekuwa inaheshimika basi uamuzi wa kuilipa au kutoilipa Dowans ungefanywa kwa pamoja.

Alisema haiwezekani dhana ya uwajibikaji wa pamoja ifanyike bila kushirikisha wengine halafu mwisho itolewe taarifa ya uwajibakaji wa pamoja.

"Halafu kuna watu wanazungumzia nimekiuka dhana ya uwajibikaji wa pamoja, uwajibikaji wa pamoja ni lazima uamuzi ushirikishe wengine si mmoja kuamua halafu ifahamike ni uwajibakaji wa pamoja," aliongeza.

Sitta pia amekuwa akihoji kasi ya malipo hayo kwa kampuni ya Dowans wakati nchi ina madeni mengine kama ya Benki ya Dunia na IMF, lakini bado hayajalipwa kwa kasi kama hiyo.

"Lakini, hii haraka ya kuilipa Dowans ni ya nini? Nchi hii ina madeni ya muda mrefu kama yale ya Benki ya Dunia na IMF, lakini hakuna uharaka wa kulipa kama huu sasa kasi hii inatoka wapi?" alihoji.

Alisema nchi ina matatizo mengi ikiwemo ya kiuchumi, hivyo haingii akilini kuona Watanzania wanalipa kiasi hicho kikubwa cha fedha kwa kampuni ya kitapeli.

Tayari msimamo wa Sitta ulimfanya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utawala Bora), Mathias Chikawe, kutoa vitisho kwa mawaziri wenzake akiwataka wakae kimya na kuacha kuzungumzia sakata hilo vinginevyo wajiondoe kwenye Serikali.

Hata hivyo, wakosoaji wamemwelezea Chikawe kama ambaye pia amekiuka taratibu kutokana na kuzungumza suala hilo kwenye vyombo vya habari, badala ya taratibu za kiserikali.

Tangu Mahakama ya Usuluhishi ya Biashara ya kimataifa (ICC Court) kutoa hukumu ya mwezi Novemba, ikitaka Tanesco ilipe Dowans, Sitta alikuwa waziri wa kwanza kupinga malipo hayo hadharani.

Hata hivyo, pamoja na Sitta kupinga, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Fredrick Werema alikwisha kusema bayana kwamba Serikali haiwezi kukata rufani katika sakata hilo, lazima ilipe faini hiyo.


3 comments:

Anonymous said...

we need such kind of people in TZ..
tukiwa nao km 10 hv tutasogea sn

Anonymous said...

Ndio watanzania wenye uzalendo tuliobakia nao! Na mimi namkubali sana Mheshimiwa!- Chriss - Sinza

Anonymous said...

TZ viongozi wote wangekuwa kama SITTA nchi ingekuwa mbali sana,neno ufisadi tungekuwa tunalisikia tuu!! Mungu ampe nguvu aendelee kulitetea taifa letu na watu wake

Website counter