|                            HAKUNA maneno yanayoweza kufaa, zaidi ya kusema  Abdallah Nyangalio ni miongoni mwa watu wenye ujasiri na uwezo mkubwa wa  kukabiliana na changamoto za maisha.   Ni jasiri kwa sababu ameweza  kupambana na ulemavu wa macho alioupata ukubwani, na badala yake  akapambana kuhakikisha anajitafutia maisha kwa njia halali, tofauti na  walemavu wengine wanaobweteka na kuishia kuwa omba omba katika maeneo  mengi, hasa ya mijini.                             |  |                               |                                                                     | Nyangalio akikata kitambaa. |  
 |                               |  |                               | 
                                                                         | Habari zinazosomwa zaidi: |                                       | 
 |  |  
 Yeye aligeukia ufundi wa nguo, na sasa ni miongoni mwa mafundi  hodari wanaokubalika ndani na nje ya nchini.  Je, ilikuwaje hata akawa  katika hali ya ulemavu aliyonayo sasa? Katika mazungumzo yaliyozaa  makala haya, Nyangalio anasema: “Nilipohitimu shule nilifanya biashara  kwa lengo la kutafuta mtaji utakaoniwezesha kutimiza ndoto za kuondokana  na umasikini, lakini niliugua na kupofuka macho hivyo kujikuta katika  kundi la watu wenye ulemavu.”
 
 Anakumbuka kwake huo ulikuwa mtihani mkubwa, lakini hakukata tamaa  ya maisha, bali alikuwa mwepesi kukubali kuishi katika hali ya ulemavu  wa macho, kisha kutafuta mbinu zitakazomuwezesha kujipatia kipato ili  kuepuka kuishi maisha tegemezi.  Uwezo wake wa kukabiliana na changamoto  za maisha ndio uliomfanya Nyangalio kuwa fundi stadi wa nguo na habari  zake zimeweza kusambaa sehemu mbalimbali Afrika Mashariki na Kati kama  kielelezo kwamba ulemavu sio mwisho wa maisha kwa kuwa mtu mwenye  ulemavu akiwezeshwa anaweza.
 
 Akielezea historia ya maisha yake, Nyangalio anasema alizaliwa mwaka  1959 katika kijiji cha Kilimani,  Rufiji mkoa wa Pwani akiwa hana  tatizo lolote la kiafya.  Alipofikisha umri wa miaka saba aliandikishwa  katika shule ya Msingi Kilimani ambapo alisoma hadi darasa la nne kisha  akahamia shule ya msingi Miburani, iliyopo Temeke jijini Dar es Salaam.   Alihitimu elimu ya msingi mwaka 1977 na kujiunga na biashara ndogo  ndogo kwa kuwa wazazi wake hawakuwa na uwezo wa kumuendeleza kimasomo.
 
 Alifanya biashara ya nguo kwa miaka kumi huku akidunduliza mtaji kwa  lengo la kufungua duka la nguo na kuimarisha biashara yake.  Hata  hivyo, anakumbuka mwaka 1988 alipata maumivu makali ya kichwa  yaliyoambatana na kukosa usingizi.  “Kichwa kiliniuma sana na nilikaa  mwezi mzima bila kupata usingizi…nilipata vidonge vya usingizi, lakini  havikusaidia badala yake kichwa kiliendelea kuuma na nikawa na hali ya  kuchanganyikiwa,” anasema.
 
 Hali hiyo ilisababisha aende katika hospitali mbalimbali kutafuta  tiba bila mafanikio hadi alipopata ushauri kwenye klabu ya Lions  iliyoambatana na barua ya kwenda katika Hospitali ya Rufaa  Muhimbili.   Baada ya kufanyiwa uchunguzi katika hospitali ya Muhimbili, Nyangalio  aliambiwa kuwa tatizo la kukosa usingizi linatokana na hitilafu  iliyojitokeza katika mishipa ya macho na tiba pekee ni upasuaji  utakaomfanya kuwa kipofu kwa maisha yake yote.
 
 “Nilielezwa wazi madhara ya kufanyiwa upasuaji na madaktari  waliniambia nina uwezo wa kukubali au kukataa tiba hiyo….kwa kuwa  niliteseka sana kwa kukosa usingizi, nilikubali kufanyiwa upasuaji,”  anasema.  Anaendelea kusema, “baada ya kufanyiwa upasuaji kichwa  kiliacha kuuma na nilipata usingizi, lakini nilipoteza kabisa uwezo wa  kuona….hata hivyo nilijipa moyo kwa kuzingatia usemi wa wahenga kwamba;  hujafa hujaumbika.”
 
 Ingawa alijipa moyo anakiri ilikuwa vigumu kukubaliana na hali hiyo  kwa sababu alishindwa kutambua mchana na usiku kutokana na kiza kinene  kilichotanda kwenye macho yake. Alihofia kuishi maisha tegemezi.  Hata  hivyo daktari aliyemfanyia upasuaji alimfariji na kumpa nafasi ya kukaa  katika hospitali ya Muhimbili kwa miezi mitatu akipewa ushauri pamoja na  mbinu za kuishi katika hali ya kutoona.  Anasema mbinu hizo ni pamoja  na elimu juu ya maisha na changamoto zinazowakabili watu wenye ulemavu  na jinsi ya kupambana nazo.
 
 Pia alifundishwa kusoma maandishi maalumu kwa watu wasioona, kutumia  cherehani pia jinsi ya kukata na  kushona nguo mbalimbali.  Baada ya  kutoka hospitalini, alikutana na changamoto nyingi katika maisha kwa  kuwa baadhi ya ndugu, jamaa na marafiki walimuona kama mzigo hivyo  baadhi ya ndugu walilumbana wakitupiana jukumu la kumtunza.  “Kabla ya  kuugua nilikuwa na mke na watoto watatu….lakini hali ya ulemavu  ilisababisha mke wangu kunikimbia kwa madai kuwa hawezi kukaa na mtu  asiyekuwa na uwezo wa kufanya kazi,” anasema.
 
 Anasema awali mke huyo aliondoka na watoto wote, lakini baadaye  aliwarudisha hivyo wakalelewa na bibi yao, yaani mama mzazi wa  Nyangalio.  “Hali ya ulemavu ilisababisha hata baadhi ya marafiki  kunikimbia….namshukuru Mungu mama yangu alinifariji, pia watoto wangu  walipoelimishwa juu ya hali yangu  walielewa, kunikubali na kunitambua  kama baba yao….jambo hilo lilinipa faraja kubwa,” anasema.
 
 Anasema pamoja visa na mikasa iliyompata aliweka mikakati ya  kushinda changamoto katika maisha ili aweze kuudhihirishia ulimwengu  kuwa binadamu ameumbwa ili aweze kukabiliana na taabu mbalimbali kwa  kumtegemea Mwenyezi Mungu.  Aliendelea kumuamini na kumtegemea Mungu kwa  kila jambo alilolifanya huku akiwa na matumaini makubwa kuwa Mungu  atampa njia nyingine ya kuishi bila ya kuwa tegemezi.
 
 Baada ya miezi saba ya ugonjwa alirudi katika shughuli za biashara  ndogo ndogo kwa kuuza nguo za mitumba pamoja na kushona nguo kwa kutumia  cherehani ya jirani yake.  Alidunduliza mtaji mpaka alipopata uwezo wa  kununua cherehani yake na kuanza kazi ya kushona nguo mbalimbali hasa  sare za wanafunzi wa shule ya msingi.  Anasema baada ya kukaa miaka  miwili bila mke, alipata mchumba na kuoa kwa kuzingatia kanuni na  maadili ya dini ya Kiislamu.
 
 Pia alijiimarisha kiuchumi na kurudia maisha ya kujitegemea kama  kiongozi wa kaya.  “Nilifarijika sana kwa kuwa mke wangu wa sasa  ananipenda kwa dhati tena alikuwa amekataa wachumba watatu na kunikubali  mimi nikiwa katika hali ya ulemavu,” anaeleza.  Anasema baadhi ya  ndugu, marafiki na jamaa wa mke wake walipatwa na mshtuko na kujaribu  kumzuia asiolewe na mtu mwenye ulemavu, lakini alishikilia msimamo wake  na kuwataka kujifunza kumheshimu Mungu ambaye ndiye anayewafanya wengine  kuishi katika hali ya ulemavu.
 
 “Msimamo wa mke wangu ulinidhihirishia ni kiasi gani anamcha Mungu,  kwani hiyo ndio sifa ya kipekee niliyoitegemea…pia mama yake mzazi  alimpa moyo wa kuolewa na mwanaume anayempenda na aliwakemea wale  waliomcheka na kumkatisha tamaa,” Nyangalio anasema.  Ingawa anakabiliwa  na hali ya ulemavu, Nyangalio ana mpango wa kutimiza shauku ya mkewe  ambaye hata kabla ya kuolewa alitamani kuwa mama wa watoto watano.
 
 “Kwa jinsi mke wangu anavyonipenda nitajitahidi kutimiza ombi lake  la kuwa na watoto watano...na Mungu akijalia mwaka huu anatarajia kupata  mtoto wa nne,” Nyangalio anasema.  Anasema atajitahidi kuitimizia  familia yake mahitaji yote, ikiwa ni pamoja na kuwapatia watoto wake  elimu bora na kuwafundisha kukabiliana na changamoto mbalimbali katika  maisha.  Kipaji cha Nyangalio alianza kufahamika mwaka 1994 wakati wa  maadhimisho ya siku ya kimataifa ya watu wenye ulemavu wa macho maarufu  kama siku ya Fimbo Nyeupe Duniani.
 
 “Wakati wa maadhimisho hayo mgeni rasmi alisifia suti aliyokuwa  amevaa aliyekuwa kiongozi wa taasisi ya wasioona. Kisha akaambiwa kuwa  suti hiyo ilishonwa na fundi asiyeona hivyo nikaanza kujulikana kuanzia  siku hiyo,” anasema Nyangalio anayekumbuka kuwashonea nguo Anna  Abdallah, wakati huo akiwa Waziri wa Afya, Sophia Simba, Joel Bendera na  wengine wengi.
 
 Hivi sasa Nyangalio anafanyia shughuli zake Mbagala Kibonde Maji  jijini Dar es Salaam ambako amejenga makazi yake ya kudumu.   Kama  ilivyo kwa Watanzania wengine, mtaji wa Nyangalio unapanda na kushuka   kwa sababu fedha kidogo anazopata katika biashara yake anazitumia kwa  mahitaji ya kifamilia, ikiwa ni pamoja na kutatua matatizo ya kijamii.   Hata hivyo, amefanikiwa kusajili kampuni inayojulikana kama Nyangalio  Fashion Centre ambayo ana mpango wa kuitumia kutoa elimu ya ufundi  cherehani hususani kwa watu wasioona.
 
 Nyangalio amewahi kutoa elimu ya ushonaji kwa watu wenye ulemavu  ambayo yalifadhiliwa na Taasisi ya Taifa ya Huduma ya Maendeleo ya  Wasioona (TNIB), ambapo wanafunzi wanne walihitimu na kufaulu kwa  kiwango cha kuridhisha.  “Wapo wanafunzi waliohitimu mafunzo ya  ushonaji, lakini hadi leo hawajaweza kutumia ujuzi wao kwa sababu ya  ukosefu wa mitaji hususani vyerehani. Tatizo hilo limenipa msukumo wa  kuanzisha kampuni ambayo itatoa fursa za ajira kwa vijana hususani wenye  ulemavu,” anasema Nyangalio.
 
 Hivi sasa ana mashine mbili za kushonea ambazo anategemea kuzitumia  kutoa mafunzo. Anaomba watu wenye uwezo kumsaidia ili kupata wafadhili  wa kutimiza ndoto zake za kuanzisha shule ya ushonaji hususani kwa watu  wenye ulemavu.  Anafahamisha kuwa watu wenye ulemavu wanatumia cherehani  za kawaida na kushona nguo kwa umakini wa hali ya juu kwa kusikiliza  mlio wa cherehani huku wakipapasa nguo ili kuepuka kupindisha.
 
 “Kwa kufuatilia mlio wa cherehani unaweza kutambua kama umetoka nje  ya mstari au la. Kwa kuwa watu wenye ulemavu wa macho hawaoni wako  makini zaidi kwa kufuatilia sauti pia kutambua vitu kwa  kuvipapasa...unajua Mungu hawezi kukunyima vyote,” Nyangalio anasema.   Hutumia umakini wa hali ya juu kupima nguo kwa kupapasa kitambaa kisha  kukipima kwa kutumia vipimo vinavyoweza kusomwa na watu wasioona.
 
 Kitu pekee ambacho mtu asiyeona hawezi kufanya ni kuchagua rangi ya  vitambaa...hapo lazima asaidiwe, lakini ana uwezo wa kutambua aina ya  vitambaa kama ni vya jinja, hariri, tetroni au polista bila kuambiwa na  mtu.  Ingawa haoni, Nyangalio ana uwezo wa kushona suti za kiume na  nguzo za kike kwa mitindo mbalimbali kiasi cha kuwazidi hata baadhi ya  mafundi wasiokuwa na ulemavu wa macho.  Wakati wa kukata nguo hutumia  sindano kuweka alama maalumu sehemu anazotaka kuweka mikunjo au vifungo.
 
 Pia hutumia mafundo madogo kama alama lakini mafundo hayo anakuwa  madogo kiasi kwamba mtu anayeona hawezi kuyatambua kwa urahisi.  Ustadi  wa Nyangalio umemuwezesha kushiriki katika maonyesho mbalimbali ya  ujasiriamali yaliyofanyika nchini pia katika nchi za Zambia na Kenya.
 
 Nyangalio anaiomba jamii kutokuwachukulia watu wenye ulemavu kama  mzigo kwa kuwa gharama za kutowaendeleza na kuwafungia ndani ni kubwa  ikilinganishwa na gharama za kuwaendeleza na kuwapa fursa ya kushiriki  katika shughuli za maendeleo ya kijamii na kiuchumi.  Pia anaiomba  serikali kutoa kipaumbele kwa watu wenye ulemavu kwa kuwapatia mafunzo  maalumu, vitendea kazi na mitaji ili kujenga jamii inayothamini utu na  changamoto zinazowakabili watu wenye mahitaji maalumu.
 
 Nyangalio ni shabiki wa michezo kama soka, anafuatilia habari za  kimataifa,  kushiriki katika masuala ya maendeleo ya jamii na  kujiendeleza kielimu.  Huyo ndiye Abdallah Nyangalio ambaye hakukata  tamaa baada ya kupata ulemavu, bali aligeuka kuwa jasiri kiasi cha sasa  kuwa mmoja wa watu wa kupigiwa mfano.  Hakuna shaka kwamba, kama atapewa  nguvu ya ziada kiushauri na hata kiuchumi, anaweza kufika mbali zaidi.  Nyangalio anapatikana na kwa simu namba 0783 399 846 au 0717 315 011.
 
 
 | 
                   
No comments:
Post a Comment