Monday, December 27, 2010

KUAPISHWA SIO HOJA ILA TUNATAKA UWAZI WA HAKI ZA KISHERIA UPATIKANE...

JK amteua Chande Othman kuwa Jaji mkuu mpya Send to a friend



RAIS Jakaya Kikwete, amemteua Jaji Mohamed Chande Othman, kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania.Jaji Othman, anachukua nafasi ya Jaji Augustino Ramadhan anayestaafu leo kwa mujibu wa sheria.

Taarifa iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu, ilisema Jaji Othman ataapishwa leo Ikulu na ataanza rasmi kazi kesho.

"Jaji Othman ataapishwa kesho (leo) saa 4:00 asubuhi, Ikulu jijini Dar es Salaam," ilisema sehemu ya taarifa hiyo iliyosainiwa na Mwandishi Msaidizi wa Rais, Premy Kibanga.

Kabla ya uteuzi huo, Jaji Othman alikuwa ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania

Jaji huyo pia amewahi kufanya kazi katika nafasi mbalimbali za kitaifa na kimataifa ikiwa ni pamoja na kuwa Makamu wa Mwendesha Mashtaka wa Mahakama ya Rwanda, iliyoko jijini Arusha.

Pia amewahi kushika nafasi sawa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali huko Timor Mashariki katika kipindi cha kati ya mwaka 2000 na mwaka 2001.

Halika kadhalika, amewahi kufanya kazi katika Shirika la Mpango wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP) na Chama cha Msalaba Mwekundu.

Mwaka 2006 Jaji Othman, alikuwa ni mmoja wa makamishna wa Baraza la Haki za Binadamu nchini Lebanon kufuatia mgogoro kati ya Lebanoni na Israel.

Novemba mosi mwaka 2009, Jaji Othman aliteuliwa kuwa mtaalamu binafsi juu ya hali ya Haki za Binadamu Kusini mwa Sudan, jukumu ambalo atalishikilia hadi Agosti mwakani.

Jaji Othman alizaliwa Januari mosi mwaka 1952 na alipata Shahada ya Kwanza ya Sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Shahada ya Uzamili (MA) katika Chuo Kikuu cha Webster, Geneva-Uswisi.

Jaji Othman anakuwa Jaji mkuu wa tano mzalendo.

Jaji wa kwanza mzalendo nchini alikuwa Jaji Agustine Said aliyekuwa anatambuliwa kama Baba wa Mahakama.

Jaji Saidi alifuatiwa na Jaji Francis Nyalali na Jaji Barnabas Samatta alikuwa Jaji Mkuu wa tatu akifuatiwa na Augustino Ramadhan, ambaye amemwachia Jaji Othman mikoba hiyo.

Juzi Jaji Ramadhan alitoa ushauri kwa mrithi wake kwamba anapaswa kujipanga ipasavyo ili matatizo mbalimbali za Idara ya Mahakama.

Akizungumza katika sherehe za kumuaga iliyoandaliwa na Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Jaji Ramadhan alisema kuna mgawanyiko mkubwa katika muhimili huo wa serikali na kwamba hali hiyo ni hatari katika utoaji wa hukumu za haki.

Akielezea uzoefu wake wa miaka mitatu na nusu kama Jaji Mkuu wa Tanzania, alisema kuendelea kuwepo kwa makundi miongoni mwa majaji, kunazidisha uwezekano wa kutotenda haki.

"Kuna baadhi ya majaji katika vyombo vya sheria ambao kati yao, kuna wanaojiona kuwa wako juu kuliko wengine na hivyo hawapendi kushirikiana na wenzao ambao bado si wazoefu, achilia mbali jamii ambayo wanaitumikia," alisema Jaji Ramadhan.

Alisema nafasi ya Jaji mkuu ni kubwa na ndio sura ya chombo cha sheria ambacho majaji waliochini yake, wanapaswa kuiga mifano yake.

Jaji Ramadhan ambaye alijielezea kama mtu anayemwogopa Mungu, alisema katika kipindi chote cha uongozi wake aliweza kujichanganya na watu wa kila aina, jambo lililomfanya agundue kuwa kuna baadhi ya majaji nchini hawatendi haki katika hukumu wanazotoa.

Alisema kuna kipindi alilazimika kuingilia kati hukumu za kesi mbili ambazo kwa mujibu wa Jaji Ramadhan, hazikuamuliwa kwa haki na kwamba hukumu hizo zilitolewa kwa ajili ya kulinufaisha kundi la watu fulani.

Jaji Ramadhan aliweka wazi kuwa kuna madudu mengi yanayofanyika kwenye Mahakama ya Rufaa kwani baadhi ya ushahidi unaotolewa huwa ni wa kupikwa na kwamba ni jukumu la Jaji mkuu kuingilia kati kila mara hali hiyo inapotokea.

Jaji Mkuu huyo alikumbushia tukio lililotokea wakati walipokuwa katika kikao kilichowakutanisha majaji wote wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa na kuelezea mtafaruku wa kurushiana maneno ulivyozuka baina ya jaji mmoja wa Mahakama Kuu na mwingine wa Mahakama ya Rufaa.

Alisema pia kuna ushirikiano mdogo miongoni mwa majaji katika mahakama hizo kubwa hapa nchini na kuelezea mfano wake alipokuwa akifanya kazi katika Mahakama ya Rufaa.

"Kama Jaji wa Mahakama ya Rufaa, baada ya kuandika hukumu nilitakiwa kuigawa pia kwa wenzangu wawili waliokuwa wakisikiliza kesi hiyo, lakini jaji mmoja alichelewa kuchukua nakala ya hukumu hiyo, na hata alipokumbushwa alionyesha kutokujali," alisema Jaji Ramadhani na kuongeza kuwa ilimbidi aipeleke nakala hiyo kwa Katibu wa Jaji huyo.

"Kama kunakuwa na hali hiyo ya kukosa ushirikiano miongoni Mwa wafanyakazi wa mahakama, unadhani haki itatendeka kirahisi," alihoji Jaji Ramadhani na kutoa wito kwa atakayeshika nafasi yake, kulishughulikia jambo hilo.

Alisema ofisi ya Jaji mkuu lazima iwe wazi muda wote na iwe inayofikika kirahisi na wananchi kwani kumekuwa na matukio mengi ya ukiukwaji wa haki katika chombo hicho.

Jaji huyo anayemaliza muda wake alisema katika kipindi cha uongozi wake, kwa kiasi kikubwa amefanikisha kuboresha uhusiano kati ya serikali, bunge na mahakama kwa sababu mihimili inapaswa kufanya kazi kwa pamoja kwa maendeleo ya nchi.

Alifafanua kuwa ili kuhakikisha uhusiano kati ya mihimili hiyo unakuwepo, aliwaalika rais na spika wa bunge kuhudhuria siku ya kimataifa ya sheria.

No comments:

Website counter