|  
 KWA muda mrefu sasa wanafunzi  katika baadhi ya vyuo vikuu nchini wamekuwa katika migomo ili  kuishinikiza Serikali  kusikiliza matatizo yao na kuyatafutia majibu.  Hivyo, wamesema kwa kuwa mamlaka husika zimetia pamba masikioni, njia  pekee iliyobaki ni kugoma, kwa maana ya kutoingia madarasani. Baadhi  ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Ardhi Dar es Salaam, wakiimba  nje ya  jingo la Utawala katika siku yao ya kwanza ya mgomo wakishinikiza  serikali kutatua  kero kumi  zinazowakabili, ikiwemo ya upungufu wa  wahadhiri na uhaba wa mabweni.
 Ni  kwa sababu hiyo tumeshuhudia habari za migomo katika vyuo hivyo  zikitawala kurasa za vyombo vya habari katika muda wa wiki mbili  zilizopita. Na katika kuchunguza kwa kina kuhusu kiini cha matatizo ya  wanafunzi hao, moja ya mambo yanayojitokeza ni kuwa matatizo hayo  yanafanana kwa kiasi kikubwa na karibu yote yanaelekezwa kwa Serikali.
       Matatizo  hayo yalianzia katika Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), ambapo  wanafunzi wa chuo hicho walivamia ofisi za bodi inayotoa mikopo kwa  wanafunzi wa elimu ya juu (HELSB), wakitaka bodi hiyo iwaongeze fedha  ili kufidia kiwango cha ada iliyoongezwa na uongozi wa chuo hicho,  lakini waliambiwa kuwasilisha malalamiko yao katika wizara husika.   Wizara hiyo ilisalimu amri na kuahidi kumaliza matatizo yao.
 
 abla  vumbi la sakata la IFM halijatulia, wanafunzi wa Chuo Kikuu cha  Kiislamu cha Morogoro na Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Kampala (Kampasi  ya Tanzania), nao waliivamia wizara hiyo kuwasilisha madai yao kuhusu  mikopo na kuambiwa kuwa Serikali ingechukua hatua kuhusu madai hayo. Na  siku tano zilizopita, wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom),   waligoma na kuzua tafrani kubwa iliyosababisha uvunjifu wa amani na  uharibifu wa mali, hatua iliyojibiwa na polisi ambao walivamia chuo  hicho na kuwapiga wanafunzi kabla hawajaondoka na viongozi wa serikali  ya wanafunzi na kuwasweka rumande.
 
 Wanafunzi hao walikuwa  wanaishinikiza Serikali iwalipe fedha za mafunzo kwa vitendo na  kutengeneza miundombinu chuoni hapo ambayo ilikuwa  katika hali mbaya,  licha ya madai yao mengine ya kuwapo uhaba mkubwa wa maji na wahadhiri.  Lakini katika hatua ya kushangaza, Serikali ilisalimu amri ambapo waziri  husika, Shukuru Kawambwa na mwenzake wa mambo ya ndani, Shamsi Vuai  Nahodha, pamoja na kuamuru kuachiwa huru kwa viongozi wa wanafunzi  waliokamatwa na polisi, walikodi ndege na kukutana na wanafunzi hao  usiku kucha katika chuo hicho, na hatimaye kuwatangazia kuwa Serikali  imekubali kutatua matatizo yao baada ya kuyaona kuwa ni ya msingi.
 
 Wakati  Serikali ikihaha kutafuta suluhisho la matatizo ya Udom, jana wanafunzi  wa Chuo cha Ardhi walianza rasmi mgomo wakiishinikiza Serikali itatue  kero zao kumi, zikiwamo uhaba wa malazi kwa wanafunzi chuoni hapo na  kushindwa kwa Serikali, kupitia bodi ya mikopo, kutangaza majina ya  wanafunzi katika chuo hicho ambao watapewa mikopo. Uongozi wa chuo hicho  unadai kuwa tayari umeipelekea bodi majina hayo wakati bodi hiyo  inakana kupokea majina hayo.
 
 Hiyo ndio hali halisi katika  vyuo vyetu vya elimu ya juu hivi sasa, na huo ndio utendaji usiowajibika  wa Serikali na vyombo vyake vinavyohusika moja kwa moja na kuhudumia  wanafunzi hao. Ni dhahiri kuwa wanafunzi wameishika pabaya Serikali  ambayo inaonekana kuwa haina pa kutokea, kwani wamechoshwa na ngonjera  za ‘ufinyu wa bajeti ya Serikali’ zinazoimbwa na vigogo wa serikali  hiyo, huku wakiendelea kununua magari ya kifahari yenye gharama ya  Sh280  milioni kila moja.
 
 Kama hali ndio hiyo, tutegemee  migomo zaidi katika vyuo vingine, kwani wanafunzi katika vyuo hivyo nao  watataka watekelezewe madai yao kama Serikali ilivyoahidi kufanya katika  vyuo vilivyogoma. Lakini kama tulivyosema katika safu hii siku chache  zilizopita, matatizo mengi katika vyuo vingi nchini yanatokana na  kukatika kwa mawasiliano kati ya wanafunzi na  uongozi wa vyuo, bodi ya  mikopo na wizara husika.
 
 | 
No comments:
Post a Comment